2014-01-28 09:39:04

Jitambueni kama Familia ya Mungu kwa kudumisha majadiliano, msamaha na upatanisho ili kujenga haki, imani na matumaini!


Katika Maadhimisho ya Sita ya kuombea amani katika Nchi Takatifu yaliyofanyika Jumapili iliyopita, tarehe 26 Januari 2014 kwa kuwashirikisha vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, waliosali na kuabudu Ekaristi Takatifu kwa muda wa masaa ishirini na manne na kuhitisha kwa Ibada ya Misa Takatifu, waamini na watu wote wenye mapenzi mema wametakiwa kujenga na kuimarisha misingi ya haki na amani.

Katika ujumbe wake kwenye Maadhimisho haya, Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani anawakumbusha waamini amri mpya upendo, ambayo inawataka kupendana kama Kristo alivyowapenda wao. Ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya kuombea amani kwa Mwaka 2014 umekuwa ni changamoto ya kujenga na kuimarisha mshikamano wa kidugu kama msingi na njia ya kujenga na kudumisha amani duniani.

Udugu ni msingi wa maisha ya upendo, amani na mapatano, ikiwa kama utafanyiwa kazi barabara. Utandawazi unaonesha kwamba, watu wako karibu, lakini kwa bahati mbaya wamemezwa mno na ubinafsi na utamaduni wa kutojali mahangaiko ya wengine kiasi kwamba; changamoto kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kujenga mshikamano wa kidugu kwa kukpokeana, kukubaliana na kusaidiana na kwamba, kwa njia ya Kristo wote wanafanyika kuwa ni ndugu wamoja; watoto wa Familia ya Mwenyezi Mungu, wanaosaidiana.

Vita, kinzani na migogoro bado inaendelea kutawala sehemu mbali mbali za dunia. Kanisa anasema Kardinali Turkson haliwezi kukaa kitako na kuangalia mambo yakienda kombo, bali litaendelea kuonesha mshikamano wa dhati na waathirika kwa kuwaonjesha upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake; kwa kuendelea kusali ili kumwomba Mfalme wa amani aweze kuwakirimia amani wananchi wanaoishi kwenye Nchi Takatifu, ili waishi kwa amani na udugu.

Wananchi watambuane kama ndugu na kusaidiana kwa hali na mali; wakijitahidi daima kufanya kazi kwa pamoja ili kufikia utimilifu wa maisha ya mwanadamu na utulivu kwa wote. Waamini wajisikie kwamba, Kanisa ni Familia ya Mungu kwa kujenga na kudumisha majadiliano, msamaha na upatanisho unaopania kujenga na kuimarisha haki, imani na matumaini. Kardinali Turkson anawataka vijana kuwa ni mashahidi wa Injili ili amani iweze kuwafikia watu wengi zaidi.







All the contents on this site are copyrighted ©.