Jeshi laanza kutoa huduma kwa wahanga wa mafuriko mkoani Morogoro
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na
Usalama, Jakaya Mrisho Kikwete ameliamuru Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kuanza
mara moja kazi ya kusimamia utoaji huduma kwa watu walioathiriwa na mafuriko katika
Mkoa wa Morogoro, ikiwa ni pamoja na kusimamia ujenzi wa nyumba za muda kwa wahanga
hao.
Rais pia ameliamuru Jeshi kupeleka mashine za kusafisha maji katika makambi
ambako wahanga hao wa mafuriko ya Januari 22, mwaka huu wanaishi kwa muda. Aidha,
Rais Kikwete amewahakikishia wahanga wa mafuriko hayo kuwa Serikali itahakikisha inawapatia
huduma zote za msingi ikiwa ni pamoja na chakula, malazi, maji na huduma za afya hadi
hapo watakapokuwa na uwezo wa kuanza kujitegemea tena.
Rais Kikwete ametoa
amri hizo kwa Jeshi Januari 27, 2014, wakati alipotembelea kambi za wahanga wa mafuriko
hayo kuwajulia hali walioathirika katika makambi yaliyoko Shule ya Sekondari ya Magole
katika eneo la Dumila na katika Kijiji cha Mateteni kilichoko Dakawa, Wilaya ya Kilosa.
Katika
hotuba zake fupi baada ya kuwa ametembelea na kuona mahema ambamo wahanga hao wanalala,
Rais Kikwete amesema ameagiza Jeshi kuongoza harakati za kuwahudumia wahanga hao kwa
sababu zikifuatwa taratibu za kawaida za Kiserikali huduma zitachelewa sana kuwafikia
waathirika. “Kazi yetu ni kusimamia maisha ya watu hasa kipindi cha shida za namna
hii. Tukifuata taratibu za kawaida za Kiserikali za tenda tutachelewesha sana huduma
za dharura kwa waathirika. Ndiyo maana nimeliamuru Jeshi kufanya kazi hii ikiwa ni
pamoja na kujenga haraka makazi ya muda kwa waathirika,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:
“Katika
mazungumzo hayo na Mkuu wa Majeshi, nimemwagiza pia kuleta mashine za kusafishia maji
ili kuhakikisha kuwa watu wanakunywa maji salama kwa sababu katika hali ya sasa maji
yasiyokuwa salama yanaweza kuwa chanzo cha magonjwa.”
Kuhusu upatikanaji wa
chakula cha msaada kwa wahanga, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali inacho chakula
cha kutosha kwa ajili yao. “Tunacho chakula cha kutosha na hata kile tusichokuwa nacho
tutanunua. Tutabanana ndani ya Serikali ili tupate fedha za kutosha za kuwahudumia.”
Kuhusu
malazi, Rais amesema:”Naambiwa kuna upungufu wa magodoro. Tutahakikisha kuwa yanapatikana
na yatafika katika siku mbili zijazo. Hatutaki watu walale chini na waje kupata vichomi.”
Kuhusu maji, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali itaendelea kutoa huduma ya maji bure
kwa wahanga. “Tutaendelea kutoa bure huduma hii mpaka hapo huduma ya kawaida ya maji
itakapoanza kupatikana tena.” Kuhusu huduma za afya, Rais amesema kuwa anafurahi kuwa
kila kambi ya wahanga inayo huduma ya afya ambayo itaendelea kutolewa kwa kadri watu
wanavyozidi kuishi kwenye makambi.
Rais ameagiza kuwa baada ya muda mfupi viongozi
wa Mkoa wa Morogoro na wilaya husika wakae chini na viongozi wa ngazi za chini na
wahanga kujadili na kutafuta mwafaka kuhusu maisha ya baadaye ya wahanga – hasa kuhusu
namna gani wanaweza kupatiwa maeneo yaliyoko nje ya mikondo ya mafuriko. “Hili ni
lazima kwa sababu hata kama imechukua miaka mingi kwa mafuriko ya sasa kutokea ni
dhahiri kuwa iko siku yatakuja tena – inaweza kuwa hata mwaka huu kwa sababu zipo
mvua za masika. Kwa hiyo ni lazima tukubaliane jinsi gani ya kurudi ama kutokurudi
katika maeneo yetu tulikotoka.”