2014-01-27 12:00:18

Wadau wa michezo simameni kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu pamoja na amani Barani Afrika!


Michezo ni chombo cha amani na ina mchango mkubwa katika mchakato wa mapambano dhidi ya baa la umaskini duniani, kama anavyobainisha Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Siku ya Kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2014.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya mawasiliano yanaiwezesha dunia kushikamana na kushirikishana karama mbali mbali kwa ajili ya mafao ya wengi. Ikiwa kama Jamii itakiuka dhamana hii kwa kujikita zaidi katika kutafuta utajiri na faida kubwa, kunahatari kwamba, michezo ikapoteza fursa ya kuwa ni chombo cha kuelimisha.

Hii ni sehemu ya ujumbe ulioandikwa na Padre Federico Lombardi, Mkurugenzi mkuu wa Radio Vatican na kusomwa kwa niaba yake na Padre Joseph Ballong, wakati wa mkutano mkuu wa saba wa Shirikisho la Vituo vya Radio Barani Afrika, uliofunguliwa tarehe 27 Januari na unakamilika tarehe 28 Januari 2014, huko Yaounde, Cameroon.

Anasema, inatia moyo kuona kwamba, Vituo vya Radio Barani Afrika vinaanza kununua leseni ya kuweza kutangaza matukio makubwa ya michezo kimataifa, lakini jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, wadau wa michezo wanasimama kidete kulinda, kutetea na kurithisha tunu msingi za maisha ya kitu na kiroho, ili kujenga Jamii inayosimikwa katika haki, amani na utulivu, kwani michezo inatumia lugha ya kimataifa inayovuka mipaka ya kidini, kikabila na kisiasa. Michezo ina uwezo wa kuwaunganisha watu, kwa kukoleza majadiliano ya kina na ukarimu.

Ni matumaini ya Padre Lombardi kwamba, michezo itasaidia kuchangia majiundo endelevu ya haki na amani Barani Afrika na kwamba, Radio Vatican itaendelea kuwa ni mdau mkuu wa utangazaji wa amani sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.