2014-01-27 08:19:32

Utengano kati ya Wakristo bado ni kashfa katika ushuhuda wa Uinjilishaji!


Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Siku kuu ya kuongoka kwa Mtakatifu Paulo, mwalimu na mtume wa mataifa, inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 25 Januari, ameongoza Ibada ya Masifu ya Jioni kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo, nje ya kuta za Roma. Ibada hii imehudhuriwa na wawakilishi kutoka madhehebu mbali mbali ya Kikristo.

Tafakari ya mwaka huu iliandaliwa na Jumuiya ya Wakristo kutoka nchini Canada, kwa kuongozwa na kauli mbiu “Je, Kristo amegawanyika?” Hii ndiyo kashfa ya utengano miongoni mwa Wakristo wanaoungama imani moja kwa Yesu Kristo mkombozi wa ulimwengu.

Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake, amewataka Wakristo kama ilivyokuwa kwa nyakati za Mtakatifu Paulo kujitahidi kuungana pamoja kwa njia ya mawazo na maneno na kwamba, umoja huu si mkakati wa kibinadamu bali ni changamoto kutoka kwa Kristo mwenyewe, anayewavuta wafuasi wake kuungana sanjari na kujiachilia mikononi mwa Mwenyezi Mungu ili aweze kutenda kadiri ya mapenzi yake yanayojikita katika upendo kwa mwanadamu. Mwenyezi Mungu ndiye kiini, sababu na kikolezo cha umoja miongoni mwa Wakristo.

Utengano miongoni mwa Wakristo si jambo la kawaida anasema Baba Mtakatifu Francisko, linalohitaji kufanyiwa marekebisho ya kina, kwani utengano kati ya Wakristo una madhara makubwa katika Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa. Unahatarisha ushuhuda unaopaswa kutolewa na Wakristo duniani.

Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanasema, Kristo ndiye msingi wa Kanisa na urithi wa wakristo wote. Lakini inasikitisha kuona kwamba, bado Wakristo wenyewe wamegawanyika kinyume kabisa cha utashi wa Kristo mwenyewe na utengano huu unaendelea kuwa ni kielelezo cha kashfa ya ushuhuda wa utangazaji wa Injili duniani.

Baba Mtakatifu anawatia shime Wakristo kufanya hija pamoja na kutegemezana ili kujenga na kuimarisha umoja miongoni mwa Wakristo. Hii ndiyo dhamana iliyotekelezwa na Papa Yohane wa XXIII na Yohane Paulo II, waliotambua umoja wa Wakristo, wakawaongoza Waamini wa Kanisa Katoliki katika hija ya majadiliano ya kiekumene, kiasi kwamba, miaka hamsini iliyopita, Papa Paulo VI akaweza kukutana na kukumbatiana na Patriaki Athenagora wa Costantinopoli.

Hii ndiyo changamoto iliyoko mbele ya Wakristo, ili kuhakikisha kwamba, wanatembea pamoja na kujenga mchakato wa majadiliano ya Kiekumene ili kufikia lengo la umoja kamili kadiri ya mapenzi ya Kristo.

Katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene, dhana ya Khalifa wa Mtakatifu Petro imejidhihirisha wazi, mwaliko wa kuendelea kufahamiana zaidi kwa ajili ya majadiliano ya Kiekumene kwa kutambua utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro, hata kwa siku za usoni.

Changamoto na vikwazo vinavyoendelea kujitokeza katika majadiliano ya Kiekumene ni mambo ambayo hayawezi kufichika, lakini kuna haja kwa Wakristo wapige kupiga moyo konde na kuanza kujivika utashi wa Kristo kwa ajili ya umoja miongoni mwa Wakristo. Wawe tayari kuvuka vikwazo vyote vinavyosababisha utengano na hivyo kujivika nguvu ya upendo inayotolewa na Roho Mtakatifu kwa ajili ya Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.