2014-01-27 08:34:07

Mshikamano wa Papa Francisko na wagonjwa wa Ukoma duniani!


Mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, Baba Mtakatifu Francisko aliwakumbusha waamini kwamba, Jumapili ya tarehe 26 Januari, Jumuiya ya Kimataifa ilikuwa inaadhimisha Siku ya Wagonjwa wa Ukoma Duniani.

Huu ni ugonjwa unaoonekana kuanza kutoweka, lakini bado unaendelea kusababisha madhara makubwa kwa watu. Jambo la msingi anasema Baba Mtakatifu ni kuendelea kuonesha mshikamano na wagonjwa wa Ukoma sehemu mbali mbali za dunia. Baba Mtakatifu anawahakikishia sala na uwepo wake wa karibu na anaendelea kuwaombea wote wanaojihusisha na huduma kwa wagonjwa wa Ukoma.

Baba Mtakatifu ameelekeza sala zake nchini Ukraine ambako kwa sasa hali ni tete kutoka na machafuko ya kisiasa na kijamii ambayo yamepelekea hadi sasa watu kadhaa kupoteza maisha na wengine kujeruhiwa vibaya wakati wa mapambano kati ya Jeshi la Polisi na wanaharakati nchini humo wanaodai Ukraine ijiunge na Umoja wa Ulaya. Baba Mtakatifu anawataka wahusika kujenga utamaduni wa majadiliano kati ya Serikali na raia pamoja na kukomesha vitendo vya uvunjifu wa amani, ili kujenga moyo wa amani kwa ajili ya mafao ya wengi.

Baba Mtakatifu Francisko amemkumbuka kwa namna ya pekee Cocò Campolongo, mtoto wa miaka mitatu aliyeuwawa kikatili miaka mitatu iliyopita kwa kuchomwa moto ndani ya gari huko Cassano, kitendo cha kusikitisha sana na mwaliko kwa wahusika kutubu na kuongoka.

Baba Mtakatifu amewakumbuka pia wananchi kutoka Mashariki ya mbali, yaani China, Korea na Vietnam wanaojiandaa kuadhimisha Mwaka Mpya. Anawatakia furaha na matumaini; umoja na mshikamano wa kidugu katika maisha ya kifamilia. Wajitahidi kujenga na kudumisha dunia inayosimikwa katika utu, ili amani iweze kutawala.

Baba Mtakatifu amemtaja Mtumishi wa Mungu Maria Cristina aliyetangazwa kuwa Mwenyeheri Jimbo kuu la Napoli. Ni Malkia wa Visiwa vya Sicilia; aliyeishi kwenye Karne ya kumi na tisa. Mwanamke aliyekuwa na utajiri mkubwa wa maisha ya kiroho, mnyenyekevu na aliyeguswa na mahangaiko ya jirani zake, kiasi kwamba, akatambulikana na wengi kuwa ni Mama wa Maskini. Hiki ni kielelezo makini cha upendo kinachoonesha kwamba, maisha ya Kiinjili yanawezekana kutolewa ushuhuda katika medani mbali mbali za maisha.

Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru kwa namna ya pekee Chama cha Vijana Wakatoliki waliokuwa wamefurika kwa wingi kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican pamoja na wazazi na walezi wao.








All the contents on this site are copyrighted ©.