2014-01-25 11:28:10

Uwajibikaji kimaadili ni jambo muhimu katika kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi!


Jumuiya ya Kimataifa haina budi kuweka mikakati makini katika masuala ya fedha na uchumi ili kukabiliana kwa dhati kabisa na changamoto ya athari za mabadiliko ya tabianchi yanayoendelea kusababisha majanga makubwa katika sehemu mbali mbali za dunia. Hili ndilo jukumu linalopaswa kushughulikiwa na wajumbe wa Jukwaa la Uchumi Duniani huko Davos, nchini Uswiss, unaofungwa rasmi tarehe 25 Januari 2014.

Jukwaa la Uchumi Duniani, lilikuwa linaongozwa na kauli mbiu "Kuleta mabadiliko duniani: athari zake kwa Jamii, Kisiasa na Kibiashara". Dr. Olav Fykse Tveit, katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anasema, Makanisa yanaunga mkono mchakato unaopania kujenga haki katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Kumbe, kuna haja kwa wanasiasa na wachumi kushirikiana kwa pamoja ili kukabiliana na athari zinazoendelea kujitokeza kabla ya mambo hayajaharibika zaidi.

Athari za myumbo wa uchumi kimataifa zilikwamisha mchakato wa Jumuiya ya Kimataifa katika kupambana na maafa yanayosababishwa na athari za mabadiliko ya tabianchi sehemu mbali mbali duniani. Mkakati huu hauna budi kuwashirikisha wadau mbali mbali kwa kuanzia kwa: Serikali, taasisi za fedha na biashara; vyama vya kiraia na Mashirika ya Kidini.

Jumuiya ya Kimataifa anasemam Dr. Tveit haina budi kurejesha tena imani na matumaini katika taasisi za kidemokrasia, ambazo nyingi kwa sasa zinaanza kupoteza dira na mwelekeo wake, kwa kutekeleza ahadi zake katika Jumuiya ya Kimataifa. Mchango wa Makanisa na Taasisi za Makanisa ni jambo la msingi, linalohitaji kuzingatia kanuni maadili na uwajibikaji katika maamuzi kuhusu taasisi za fedha na biashara.

Wadau mbali mbali wanaendelea kuyapongeza Makanisa kwa kuhamasisha utunzaji bora wa mazingira kama sehemu ya mchakato wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi yanayoendelea kusababisha majanga makubwa sehemu mbali mbali za dunia. Lengo ni kuiwezesha Jamii kudumisha haki katika masuala ya mabadiliko ya tabianchi.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bwana Ban Ki-Moon amewahimiza viongozi wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa pamoja na Taasisi za Fedha na Biashara kushikamana katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.







All the contents on this site are copyrighted ©.