2014-01-25 07:59:39

Cheche za mafanikio ya majadiliano ya kiekumene zaanza kuonekana!


Je, Kristo amegawanyika? Ndiyo kauli mbiu inayoongoza Maadhimisho ya Juma la Kuombea Umoja wa Wakristo kwa Mwaka 2014. Kardinali Kurt Koch, Rais wa Baraza la Kipapa la kuhamasisha Umoja wa Wakristo anabainisha kwamba, majadiliano ya kiekumene yameendelea kupewa kipaumbele cha pekee na Kanisa Katoliki tangu baada ya Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Kanisa ambalo kimsingi ni: moja, takatifu, katoliki na la mitume, kwa asili linajikita katika umoja wa Fumbo la Mwili wa Kristo, lakini kwa bahati mbaya, bado kuna utengano miongoni mwa wafuasi wa Kristo, jambo ambalo ni kashfa. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican waliiona na kusikitishwa na kashfa hii inayoendelea kujionesha miongoni mwa Wakristo.

Ndiyo maana, Miaka 50 iliyopita, Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wakachapisha hati kuhusu majadiliano ya Kiekumene inayojulikana kwa lugha ya Kilatini kama “Unitatis Redintegratio”, ambayo mwaka huu inaadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu ilipochapishwa. Wakristo wanatamani kuona Kanisa la Mungu moja na linaloonekana, liwe kweli ni kwa ajili ya wote na linalotumwa duniani kutangaza Habari Njema ya Wokovu, ili watu waweze kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu na hatimaye, kupata ukombozi ambao ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Mgawanyiko miongoni mwa wafuasi wa Kristo ni jambo ambalo linakwenda kinyume cha mapenzi ya Kristo mwenyewe aliyewaombea wafuasi wake wawe wamoja kama Yeye na Baba yake wa mbinguni walivyo wamoja! Kardinali Koch anasema, utengano miongoni mwa Wakristo unachafua utakatifu wa maisha ya Kanisa na kuvuruga ushuhuda wa utangazaji wa Injili ya Kristo kwa watu wa Mataifa. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican waliona na kutambua kwamba, majadiliano ya kiekumene ni kati ya vipaumbele vya Kanisa Katoliki katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Kanisa Katoliki linatambua na kuthamini dhamana na utume wa majadiliano ya kiekuemene mintarafu uelewa wa Kanisa kama Mababa wa Mtaguso mkuu wa Vatican wanavyofafanua kwa kina katika hati juu ya Kanisa, Lumen Gentium, yaani Mwanga wa Mataifa.

Kuna uhusiano wa dhati kati ya Kanisa na Majadiliano ya Kiekuemene, kwani hii ni hija ambayo Kanisa Katoliki linapania kusaidia mchakato wa kujenga na kuimarisha umoja miongoni mwa Wakristo katika uhalisia wa maisha na wala si katika dhana wala wazo la kufikirika. Hati juu ya Kanisa inafafanua kwa kina na mapana mwelekeo huu wa maisha.

Kardinali Kurt Koch anabainisha kwamba, Papa Paulo VI katika hotuba yake ya ufunguzi wa Awamu ya Pili ya Maadhimisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican alikazia kwa namna ya pekee, umuhimu wa majadiliano ya kiekumene katika maisha na utume wa Kanisa, kwa kuwa na mwelekeo mpana zaidi kuhusu ufahamu wa Kanisa ili kuanzisha mchakato wa kuponya madonda ya utengano miongoni mwa Wakristo. Hati ya Majadiliano ya Kiekumene ilipewa uzito wa pekee sanjari na kuongeza jitihada za majadiliano ya Kiekumene na Makanisa ya Mashariki pia.

Papa Paulo VI anasema kwamba, majadiliano ya Kiekumene ni hija ya Mama Kanisa, kama anavyokazia Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili katika hati yake ya kichungaji, ili wote wawe wamoja, Ut Unum Sint. Huu ni mchakato wa maisha na utume wake, kwa kuendelea kuwa makini ili kusikiliza sauti ya Roho Mtakatifu kwa Makanisa pamoja na kusoma alama za nyakati.

Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI akaivalia njuga changamoto ya majadiliano ya Kiekumene katika mikakati na vipaumbele vyake kwa maisha na utume kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hii inatokana na ukweli kwamba, majadiliano ya Kiekumene yanapata chimbuko lake kutoka katika asili ya utume wa Kanisa lenyewe. Ni mchakato unaofumbatwa katika uhalisia wa maisha katika imani.

Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa kitume, Injili ya Furaha, Evangelii Gaudium anasema kwamba, majadiliano ya Kiekumene si sehemu ya mchakato wa shughuli za kidiplomasia au jambo la kulazimishana, bali ni changamoto ya kufanya toba na wongofu wa ndani, ili Wakristo kwa pamoja waweze kushikamana katika kutangaza Injili ya Furaha, ili ushuhuda wao uweze kuwa na mvuto pamoja na mashiko.

Huu ndio mwendelezo wa Mafundisho wa Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika mchakato wa majadiliano ya Kiekumene. Hati za Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kuhusu: Kanisa, Majadiliano ya Kiekumene na Makanisa ya Mashariki ni muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa, katika mchakato wa ujenzi wa Umoja wa Kanisa la Kristo.

Kardinali Kurt Koch anaendelea kufafanua kwamba, Sheria za Makanisa ya Mashariki, zilizoidhinishwa na Mwenyeheri Yohane Paulo II kunako Mwaka 1990 ni matunda ya mchakato wa majadiliano ya Kiekumene na Makanisa ya Mashariki ili kuweza kupata umoja kamili miongoni mwa Wafuasi wa Kristo. Ni mwaliko na changamoto ya kufanya hija ya toba, wongofu wa ndani na upatanisho wa kweli.

Ni matumaini ya Kanisa Katoliki kwamba, mwaka huu 2014 katika Jubilee ya Miaka 50 tangu hati ya Majadiliano ya Kiekumene ichapishwe na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, hatua kubwa zaidi zinaweza kutekelezwa na Makanisa, ili kuponya kashfa ya utengano kati ya Wakristo. Mwaka 2017, Makanisa ya Kiluteri yatakuwa yanaadhimisha Jubilee ya Miaka 500 tangu yalipofanya mabadiliko makubwa ndani ya Kanisa.

Huu ni mwaliko wa kutoka katika hali ya kudhaniana vibaya na kuanza mchakato wa ujenzi wa Umoja wa Kanisa, kwa kujikita zaidi katika mambo yanayowaunganisha Wakristo katika maisha na imani pamoja na kujitahidi kuponya majeraha ya utengano yaliyojitokeza miaka 500 iliyopita.

Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kukutana na kuzungumza na Patriaki Bartholomeo wa kwanza wa Kanisa la Kiorthiodox la Costantinopoli, kama kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana na kuzungumza na Patriaki Athenegoras Januari 1964. Huu ni mchakato wa majadiliano ya Kiekumene yanayojikita katika Upatanisho, ili kuungama Imani moja kwa Kristo na Kanisa lake. Wakristo wanakumbuka kwa namna ya pekee Mwaka 1054, uliopelekea utengano ulioleta ubaridi katika upendo, umoja na mshikamano kati ya Wakristo.

Kardinali Kurt Koch anatumaini kwamba, majadiliano ya Kiekumene yanayoendelea kutekelezwa kati ya Patriaki Bartolomeo wa kwanza na Baba Mtakatifu Francisko yataweza kuwasha moto mpya wa umoja na mshikamano wa dhati miongoni mwa Wakristo hasa kwa Wakristo kuadhimisha kwa pamoja Fumbo la Ekaristi Takatifu, uwepo endelevu wa Kristo ndani ya Kanisa lake. Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican unaendelea kuwa ni nguzo msingi katika mchakato wa majadiliano ya Kiekumene miongoni mwa Wakristo.








All the contents on this site are copyrighted ©.