2014-01-23 10:20:07

Wakimbizi 26, 000 kurudishwa nchini Angola Mwaka 2014


Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR limeonesha mpangomkakati wa kutaka kuwarudisha nchini mwao, wananchi 26, 000 kutoka Angola waliokua wamekimbilia Zambia, Afrika ya Kusini, DRC na Bostwana ili kupata hifadhi wakati wa vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Angola.

Shirika la kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa linaendelea kushirikiana na Serikali ya Angola ili kuweka mikakati makini kwa ajili ya kuwapokea wananchi wa Angola wanaorudi nchini mwao baada ya amani na utulivu kuanza kushika hatamu. Inakadiriwa kwamba, kila juma, zaidi ya wakimbizi 1, 200 watakuwa wanarudishwa Angola katika eneo la Uige.

Umoja wa Mataifa unafafanua kwamba, kwa wananchi wa Angola ambao wataridhia kubaki katika nchi zile ambazo ziliwapatia hifadhi wakati wa vita wako huru na watapatia uraia na wale wanaorudi watafanya hivyo kwa hiyari yao bila shuruti. Ufafanuzi huu umetolewa na Bwana Hans Lushof, Mwakilishi wa UNHCR nchini Angola.

Takwimu zinaonesha kwamba, vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Angola kuanzia Mwaka 1961 hadi mwaka 2002, ilipelekea watu zaidi ya millioni nne kuikimbia Angola ili kuokoa maisha yao. Kuna wakimbizi laki sita wanaoendelea kupata hifadhi katika nchi jirani na Angola.







All the contents on this site are copyrighted ©.