Umuhimu wa Muziki mtakatifu katika Liturujia ya Kanisa
Hivi karibuni Jimbo kuu la Dar es Salaam kwa kushirikiana na Idara ya Liturujia ya
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania liliendesha semina maalum ya walimu wa nyimbo,
Jimbo kuu la Dar es Salaam na kuhudhuriwa na: Pd Paterni P. Mangi – Katibu Mtendaji
Idara ya Liturujia, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Uongozi wa Shikwaka Jimbo
Kuu Dar es Salaam. Waalimu 108 wa kwaya kutoka katika Parokia za Jimbo Kuu la Dar
e Salaam. Ifuatayo ni tathmini ya Walimu wa Kwaya Jimbo Kuu la Dar es Salaam juu
ya Kuuboresha Muziki Mtakatifu wa Kanisa Katoliki la Tanzania. AGENDA 1. HALI
YA MUZIKI WA KANISA KWA SASA Katika kipindi cha miaka mitano hivi iliyopita muziki
wa Kanisa umebadilika na umepitia katika mambo mengi sana baada ya kuibuka kwa vipaji
vipya vya utunzi na upigaji kinanda. Hali hiyo imesababisha asili ya muziki wa Kanisa
kwenda mrama na kutawaliwa sana na muziki wa mapambio; yaani watunzi wametoka kwenye
mwelekeo na maelekezo ya Kanisa katika kutunga nyimbo. 2. KUHUISHA MUZIKI KATOLIKI
TANZANIA 2.1 Mababa wa Kanisa Tanzania wamegundua hili na jitihada za makusudi
zimeanza chini ya kitengo cha Liturujia TEC ngazi ya taifa ili kuunusuru muziki mtakatifu
wa Kanisa Katoliki. 2.2 Hivi ili kurudisha hadhi ya muziki wa Kanisa na mwelekeo
wa watunzi wetu, zinahitajika semina nyingi zaidi. Semina za walimu wa kwaya katika
jimbo kuu la Dar es Salaam ziwe endelevu na zifanyike mara kwa mara ili walimu tutambue
nafasi zetu na wajibu wetu katika Kanisa na jamii kwa ujumla. 2.3 Kuundwa kwa chombo
maalumu ambacho kitafanya sensa ya nyimbo zote, na kwa kufuata vigezo vitakavyowekwa.
Chombo hicho kipewe mamlaka ya kuziondoa nyimbo zisizofaa ili zisitumike katika ibada.
Hii ni Kutokana na kuwepo kwa utitiri wa nyimbo nyingi kwa sasa. Azimio hilo baadaye
lipewe baraka na kitengo cha liturujia ngazi ya taifa kwa utekelezaji wake. 3.
UPATIKANAJI WA NYIMBO ZILIZOKWISHACHAPWA Kutengenezwe tena vitabu vya nyimbo kama
vile vya NL 1&2 vilivyotolewa awali. Hata hivyo hatuna budi kujifunza na kutokurudia
makosa ya matoleo ya awali, kama vile:- i. Toleo NL 1 lilikosewa sana kwani
lilikusanya nyimbo za ukanda wa Kusini tu, pia majina ya watunzi wa nyimbo husika
hayakuwekwa. ii. Japo Toleo NL II lilikuwa na mabadiliko makubwa, katika matoleo
yajayo inashauriwa yawe bora zaidi, kiusahihi wa kunakili nyimbo bila makosa na pia
kwa kuwa makini na aina gani ya nyimbo zinawekwa. Kwa mfano unawekwa wimbo mpya wa
“ Bwana ndiye mchungaji wangu”, ambao haujullikani kama ule wenye maneno kama hayo
uliotungwa na mtunzi na gwiji la muziki Mwalimu John Mgandu. iii. Baraza la Maaskofu
kupitia kitengo chake cha liturujia kiwe na utaratibu mzuri wenye wigo mpana wa uwakilishi
na ushirikishi wakati wa kuandika vitabu hivi. 4. UTAMADUNISHO WA SINODI YA AFRIKA
Dhana ya utamadunisho iliyotolewa katika Sinodi ya Afrika inahitajika kutafsiriwa
upya kwa watu ili waelewe mipaka yake, kwani suala hili halijaeleweka kwa watu hadi
sasa, wengi wakidhani kuwa utamadunisho ni kucheza Kanisani wakati wa kuimba! 5.
WALIMU WA KWAYA – MAJUKUMU, MIPAKA NA SUALA LA ITHIBATI 5.1 Mipaka ya Utendaji
kazi Walimu walio wengi hawajui mipaka yao katika utendaji wa kazi zao za kila siku
za utume katika nyanja nyingi:- 5.1.1 Kiutawala: Wajibu wa walimu umeainishwa vema
katika katiba za kwaya zao husika. Hivi mwalimu kuingilia suala jingine zaidi ya wajibu
wake ni kuvuka mipaka na kuleta fujo katika vikundi. 5.1.2 Kiutunzi: Walimu wengi
hubadilisha matini za nyimbo za liturujia (“matini” ni maneno ya nyimbo kadiri ya
vifungu vya Biblia), na kuweka maneno yao ambayo si ya Biblia lakini pia yenye kuleta
tafsiri potofu na tofauti na muziki mtakatifu wa Kanisa Katoliki. Kwa mfano maneno
ya nyimbo / maneno kama vile:- a. Mchanganyo Bwana Yesu amekataa, b. Shetani
kapata pancha safari haiendelei, na ule c. Nimevunja mkataba na shetani d.
Kutumia maneno mepesi (circular words) kama vile “Yesu kavalishwa nepi” badala
ya “Yesu kavalishwa mavazi ya kitoto”
5.2 Walimu kukosa moyo wa ibada wawapo
Kanisani. Walimu inabidiwafundishane kwa upendo elimu ya muziki badala ya kushindana
bila sababu. 5.3 Upigaji wa kinanda:Wapigaji vinanda wameshindwa kutambua mipaka
yao ya taalamu, mfano:- 5.3.1 Wapo wanaopiga chords tu kwa kukosa kufanya mazoezi
ya nyimbo husika. 5.3.2 Wapo wanaotoa tuni ya wimbo mwingine, wakati wimbo utakaoimbwa
ni mwingine. 5.3.3 Wapo wanaopiga tuni za nyimbo za mitaani (kwa mfano, Kamongo
au mapambio ya ndoa) na tuni za nyimbo nyingine kwenye free organ ya wimbo husika
wakati wa maadhimisho ya liturujia. Kimsingi hali hii inaonyesha ni namna gani wapiga
vinanda walivyoishiwa kiutaalamu na hivi kuharibu uzuri wa muziki wa Kanisa Katoliki. 5.4
Wapo walimu wengi sana katika kwaya zetu ambao hutanguliza mbele matakwa yao wenyewe
badala ya kufuata nini Kanisa linataka. 6 MAPAROKO NA VIONGOZI WALEI WA PAROKIA 6.1
Baadhi ya migogoro katika kwaya kwa kiasi kikubwa huchangiwa na maparoko na viongozi
wa parokia zetu. Ni dhahiri kuwa wapo mapadre leo ambao tangu walipokuwa seminarini
walikuwa hawapendi muziki, na kitu chochote wanachofanya wanakwaya, hata kama kiwe
kizuri kinakuwa kosa. Imezoeleka sasa kuwa padre kuzuia kwaya isiimbe wimbo fulani
au kuisimamisha kwaya isitoe huduma ni kitu cha kawaida. 6.2 Kitengo cha liturujia
kiangalie namna ya kuweka utaratibu elekezi ambao utawasaidia maparoko kutoathiri
utume wa uimbaji ambayo nao una nafasi kubwa sana katika kuihubiri Injili. Pamoja
na changamoto hizi, walimu wa kwaya tuendelee kutumia busara kwa kupokea na kurekebisha
maagizo tunayopewa na hirakia za Kanisa mahalia. 6.3 Mapadre wanapaswa kuwaonyesha
wanakwaya upendo kwani nao wanafanya kazi ya kuhubiri injili na kumsaidia padre katika
maadhimisho ya misa. Pia mapadre wengi wanapenda kuendesha misa haraka haraka sana
kama vile kuna kitu wanakimbilia baada ya misa. Hali hiyo inasababisha mapadre kuzuia
kwaya isiimbe Bwana Utuhurumie na Utukufu hata siku za Jumapili (Solemnity) tena bila
kufanya mawasiliano na kwaya hivi kuharibu uzuri (decorum) wa ibada. Katika maisha
ya sasa yenye changamoto kubwa za kiuchumi, wanakwaya hujitolea kwa moyo muda wao
kwa ajili ya utume wa uimbaji hivyo Maparoko wanapaswa kuheshimu majitoleo hayo na
hivyo kutoa ushirikiano na mawasiliano muafaka iwapo ratiba za ibada zinabadilika.
Hii itafanya wanakwaya kutokuona wanapotezewa muda wao kwa mazoezi mengi walakini
ibada inakatwakatwa sehemu za nyimbo. 6.4 Uelewa juu ya muziki wa Kanisa Katoliki
usiishie tu kwa walimu bali ufikishwe pia kwa wanakwaya ili nao kama wadau waelewe
maana yake na jinsi wanavyoweza kuutofautisha na miziki mingine. 7 TATIZO LA KIWANGO
KIDOGO CHA ELIMU YA MUZIKI KWA WALIMU 7.1 Kurejea mada ya semina, mwalimu anatakiwa
aweze kutofautisha kati ya muziki unaostahili kuimba Kanisani na ule wa mapambio unaostahili
kuimbwa nje ya ibada na katika majukwaa. Ikitokea kuna mwalimu asiye na uelewa huo
na akakutana na wanakwaya wenye uelewa kama wa kwake, muziki utakaoingizwa katika
maadhimisho ya ibada utakuwa nje ya mwongozo wa ibada. Walimu wanatakiwa kujielimisha
kwa kiwango kikubwa kimuziki na liturujia ili kuweza kuongoza kwaya. 7.2 Sio kila
wimbo unaotungwa unaweza kukubalika. Watunzi wanaochipukia wajifunze toka kwa muziki
uliotungwa na watunzi wa zamani (waliopumzika katika amani ya Bwana) kama vile: Padre
Gregory Kayetta , Padre Daudi Ntampambata , Padre Stefano Mbuga , Felician Nyundo,
John Mgandu, Joseph Makoye, Elias Kalluh, Joseph Mkomagu, Isaya Nganga Stansalus
Mujwahuki, na wengine wengi. 7.3 Na pia kwa watunzi wasasa ambao muziki wao bado
unatunza hadhi na maadili ya muziki wa Kanisa Katoliki kama vile: Padre Lui Mwanampepo,
Charles Saasita, Venant Mabula, Beatus Idama, Dismas Mallya, Fortunatus Mallya,
Faustine Mtegeta, Robert Kawite, David Wasonga, Benedict Simfukwe, n.k. Kujifunza
toka wanamuziki hawa itasaidia sana katika jitihada za kurudisha hadhi ya muziki wa
Kanisa Katoliki Tanzania. Kikubwa hapa mwalimu anapaswa kuuvaa unyenyekevu kama wa
Baba wa Kanisa Bonaventura aliyeichana kazi yake aliyoiandaa kabla hajaisoma kwa Baba
Mtakatifu wa wakati ule, si kwa vile haikuwa na ubora bali kwa unyenyekevu aliheshimu
kazi ya Thomas wa Akwino aliyoisoma mbele ya Baba Mtakatifu na ilikuwa na ubora mkubwa
juu ya sifa za Ekaristi Takatifu. Unyenyekevu gani huu mkubwa ambao leo tunaweza kuuiga? 8
NINI KIFANYIKE SASA 8.1 Ni kazi kubwa sana kuurudisha ubora wa muziki wa Kanisa
Katoliki. Ni wazi kuwa kwaya nyingi sasa zinaimba na kurekodi nyimbo za kisasa kutokana
na soko lao la wakati huu lilivyo, na hii inatokana na wanamuziki wengi kuiga muziki
wa dunia (taarabu, jazz, blues, sebene n.k) kinyume na muziki wa historia ya Kanisa
(sacred and solemnal, liturgical). Hata Papa Pio X mwaka 1903 alitoa mwongozo juu
ya muziki mtakatifu wa Kanisa Katoliki (Tra le Sollecitudini Instaurare Omnia in
Cristo). kwa lengo la kuurekebisha muziki wa Kanisa. Hivyo kwa kuanzia: 8.1.1
Waamini waelimishwe juu ya mkakati huu wa kurudisha muziki wa Kanisa Katoliki. 8.1.2
Mapadre na maaskofu ambao baadhi yao ni mashabiki wakubwa wa miziki hiyo nao waelimishwe
juu ya nia hii ya Kanisa. 8.1.3 Baraza la Maaskofu, chini ya kitengo chake cha
liturujia lije na mikakati mahususi katika kutekeleza azma hii. Kwa mfano ni namna
gani Kanisa litaufanya muziki wa kisasa kuwa na sura ya kikatoliki. 8.2 Ili kudhibiti
ubora wa nyimbo, itengenezwe tovuti ya SHIKWAKA jimbo kuu la Dar es Salaam, ambapo
marekebisho au ushauri utakuwa rahisi kutolewa. 8.3 Redio za Kanisa zitusaidie
katika kuelezea uma juu ya nini maana ya muziki wa Kanisa Katoliki, na pia kwa kupiga
katika redio hizo nyimbo zile za muziki wa Kanisa Katoliki. 9 MOYO WA KUJIFUNZA Uwepo
wa wana muziki wenye umri na ambao wamekuwa katika tasnia ya muziki wa Kanisa kwa
siku nyingi walihudhuria semina hii. Hili ni jambo la kujifunza toka kwao hasa kwa
wanamuziki wanaochipukia ambao wengi wao wanaona tayari wamefikia upeo katika muziki.
Tumeona vema kutambua baadhi ya wanamuziki hao waliohudhuria semina hii ili tujifunze
na kuongeza elimu ya muziki kutoka kwao katika tasnia hii ya muziki kwa ujumla. Hao
ni kama:- a. Benedict Simfukwe, b. Robert Kawite, c. Faustine Mtegeta, d.
Mwalimu Kanuti, e. Justine Ncheye, f. Fortunatus Mallya, na g. Dismas Mallya. Pia
katika semina hii walihudhuria wataalamu wa muziki wa pekee (classics) ambao wanaendesha
kikundi cha muziki kijulikanacho kama The Dar Choral Society. Muziki huu wa pekee
(classical music) unahitaji nidhamu ya hali ya juu na moyo wa kujituma. Baadhi ya
miziki inayopigwa na kikundi hiki huimbwa pia Kanisani nyakati za maadhimisho kama
Aleluya Kuu na miziki mingine iliyotungwa na George Frederick Haendel,
Misa iliyotungwa na Wolfgang Amadeus Mozart , Johann Sebastian Bach, n.k. Wataalamu
wa muziki huo waliohudhuria semina hii ni: a. Raymond Hekima, na b. Paschal
Mhangamkali Gunganamtwa Kwa wanamuziki hawa licha ya uzuri wa kazi zao walizozitoa
katika muziki bado wanaitikia kuja katika semina hizi na wamechangia mawazo katika
kuboresha muziki wa Kanisa. KINANDA Kwa wapiga kinanda, ilishauriwa kuwa watenge
muda wao wa kutosha kwa ajili ya kufanya mazoezi na si kufanya mazoezi wakati wa ibada.
Tena watumie vitabu vya mwongozo ya majifunzo ya Kinanda, mf. Kitabu cha Harmonium
Schule kilichotungwa na Heinrich Bungart, na vitabu vingine kama hivyo, kwani kupiga
Kinanda ni sanaa, na sanaa yoyote ili iwe nzuri ni lazima kujifunza na kufanya mazoezi
mara kwa mara: Practice makes perfect. 10 Nyimbo za zamani na Gregorian chants 10.1
Hizi ni hazina ya Kanisa hivyo zinapaswa kufundishwa katika kwaya zetu. Yapo makanisa
machache ambapo WIMBO WA KATIKATI una tuni moja tu inayotumika katika ibada zote mf.
Parokia ya St. Peters, Oysterbay, hii inatoa ushiriki wa waamini wote kuimba kiitikio
hicho. 10.2 Pia desturi ya kufundisha nyimbo za Kilatini katika kwaya zetu ni suala
ambalo walimu inabidi tutilie mkazo ili ikiwezekana ndani ya mwezi kuwe na dominika
moja ambayo nyimbo hasa Ordinarium (nyimbo zisizobadilika kila ibada) zitaimbwa kwa
Kilatini. 11 UBORESHAJI WA NYIMBO ZA ZAMANI 11.1 Vipo vikundi vya muziki zikiwemo
kwaya ambazo zinabadili nyimbo za zamani kwa kuweka vionjo vipya vya muziki kwa kuingiza
midundo ya ngoma na hivi kuharibu uzuri wa awali wa wimbo husika. Hapa mfano umetolewa
wa kikundi KAPOTIVE SINGERS, BUKOBA ambao wameubadili wimbo wa “ PENDO LAKO YESU LIMENIVUTIA
NIWE WAKO MILELE ” na hivi kusikika tofauti kabisa na asili yake. 11.2 Pia zipo
kwaya zinazoweka ngoma katika Gregorian chants. Kwa mfano, “Christus Vincit”, kitu
ambacho hakikubaliki. Nyimbo hizi zinaimbwa bila ngoma. 12 MISALE YA KIRUMI Utaratibu
wa kufuata Misale ya Kirumi haujaeleweka na ipo haja ya kuwa na mwongozo wa pamoja
kwa parokia zote. 13 Idadi ya walimu wa kike katika semina walikuwa watatu tu kati
ya walimu wa kiume 108 waliohudhuria. Akina dada na kina mama ambao ndio wanachukua
asilimia kubwa sana katika kwaya zetu wahamasishwe katika kujifunza muziki. MAAZIMIO: 1.
Semina nyingine ambayo itakuwa ya ukubwa zaidi itafanyika kabla ya kuanza kwa Kwaresma
na itahusisha: a. Masomo juu ya nadharia ya sheria za utunzi, harmony n.k b.
Uimbishaji wa kwaya (Conducting patterns) c. Upigaji wa Kinanda (Keyboard playing) 2.
Semina hizi pia zipelekwe kwenye majimbo mengine. 3. Miongozo ya sheria zinazotakiwa
katika utunzi wa muziki mtakatifu wa Kanisa Katoliki zitatolewa kwa walimu 4. Tathmini
ya walimu itatolewa katika magazeti ya Kanisa Katoliki na kutangazwa katika redio
za Kanisa katika vipindi maalumu. 5. Kuundwa kwa kamati maalum za kiliturujia zikijumuisha
walimu. 6. Kwaya zirudishe desturi ya kutunga nyimbo za kiliturujia: Misa, Zaburi,
Sadaka, Komunio, Shukrani, Tafakari n.k. badala ya kuimba nyimbo za mapambio ili kuivutia
hadhira. Tena uzoefu unaonyesha kuwa walimu wengi wa kwaya huwa wanawafundisha nyimbo
wanakwaya kwa ajili ya kurekodi hivyo mwanakwaya hukosa nafasi ya kuhoji aina ya nyimbo
wanazofundishwa. UCHUNGUZI KIFANI (CASE STUDY) Kuna kwaya ilienda kurekodi katika
studio ambapo wataalamu wa kurekodi, “sound engineers” ni wakristo wa madhehebu yasiyo
ya Kikatoliki. Baada ya kurekodi nyimbo na wakiwa wanaelekea kumaliza kurekodi walirekodi
wimbo wa marehemu Nganga wa, “Nimrudishie Bwana nini kwa ukarimu wake wote…”, wale
wataalamu wakasema kwa mshangao, “Loo! Hatimaye kwaya hii sasa imerekodi wimbo wa
Kikatoliki!” Kuacha desturi ya kuimba nyimbo za Kanisa Katoliki hushtua hata watu
wengine na si Kanisa Katoliki tu. Kumbe ni vizuri kubaki katika reli kama alivyoshauri
mwanamuziki mmoja mkongwe. Hivyo basi:- 1. Ithibati: Nyimbo za kurekodiwa zipitishwe
kwa kamati ya liturujia jimbo ili kupata kibali. Hata kama padre mhusika hajui muziki
lakini atasaidia katika kushauri juu ya maneno yaliyotumika yasije yakaleta mafundisho
ya kukufuru (profanity). 2. Katika kujifunza jinsi kazi za muziki zilivyo, walimu
wapate muda wa kuhudhuria “concerts” ambazo mwalimu Raymond Hekima anaziandaa. Kuna
mengi mazuri ya kimuziki yatapatikana. 3. Katika hatua za kurudisha tungo za muziki
wa Kanisa Katoliki, zinakusanywa nyimbo za wanamuziki waliotutangulia mbele ya Bwana
kama vile: Felician Nyundo, John Mgandu, Joseph Makoye, Elias Kalluh, Joseph Mkomagu,
Isaya Nganga, Stansalus Mujwahuki, Antony Sing’ombe, Guido Matui na wengine na kutengeneza
vitabu vya nyimbo zao. HITIMISHO Muziki mtakatifu wa Kanisa Katoliki ulioharibiwa
utarudishwa na walimu wa kwaya kwa ujumla. Katibu Mtendaji wa Idara ya Liturujia ngazi
ya Taifa, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Fadre Paterni Mangi anatambua
kuwa asilimia kubwa ya muziki wetu umeharibika na ana nafasi kubwa ya kurudisha hadhi
yake na ametangaza kuwa safari ya kuurudisha muziki wa Kanisa Katoliki imeanza sasa
na anaomba tushirikiane sote katika kurejesha hadhi ya muziki wa Kanisa Katoliki. Imeandikwa
na:- 1. Francis Mhagama, na 2. Justine Ncheye Na kuhakikiwa na:- Pd. Paterni
P. Mangi - Katibu Mtendaji Idara ya Liturujia – TEC 03.12.2013 DAR ES SALAAM