2014-01-23 09:39:15

Papa Francisko anafuatilia kwa makini na masikitiko makubwa yale yanayoendelea kutendeka Sudan ya Kusini


Askofu mkuu Charles Daniel Balvo, Balozi wa Vatican Sudan ya Kusini anasema, Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kufuatilia kwa makini machafuko ya kisiasa nchini Sudan ya Kusini yaliyopelekea watu wengi kupoteza maisha na wengine kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wao. Anawaalika viongozi wa Serikali na Kisiasa kuweka silaha chini na kuanza mchakato wa majadiliano yanayopania upatikanaji wa amani ya kudumu.

Askofu mkuu Balvo ameyasema hayo mapema juma hili, alipowasili mjini Juba ili kushiriki katika mkutano maalum wa Baraza la Maaskofu Katoliki Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini, unaoendelea hadi tarehe 30 Januari 2014. Askofu mkuu Balvo anawaalika vijana na wananchi wenye mapenzi mema Sudan ya Kusini, kujikita katika amani na mapatano ili kuondokana na falsafa ya vita inayoendelea kusababisha maafa makubwa katika Jamii.

Askofu mkuu Balvo anawapongeza Maaskofu kwa kuendelea kushikamana na kujitoa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Sudan katika ujumla wake. Anawaalika viongozi wa Kanisa kuwa kweli ni mashahidi wa Injili ya Kristo hata katika mazingira magumu kama yanavyojionesha nchini Sudan ya Kusini.

Neno la Mungu ni ujumbe wa matumaini na mapendo, unaojikita katika imani, ujasiri na nguvu, changamoto kwa Maaskofu kuwashirikisha Wakristo wao Injili ya Furaha na Amani, kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili.







All the contents on this site are copyrighted ©.