2014-01-22 08:31:19

Msiogope! Ishuhudieni imani kwa ujasiri! Uwepo wenu Zanzibar si ajali!


Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inakuletea hotuba ya Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 150 ya Uinjilishaji endelevu Jimbo Katoliki Zanzibar, Jumapili tarehe 19 Januari 2014 iliyosomwa kwa niaba yake na Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu Katoliki Arusha.

Ibada ya Misa Takatifu iliongozwa na Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam. Familia ya Mungu Jimbo Katoliki Zanzibar imetakiwa kufanya tafakari kwa kujiuliza ni kitu gani kilichofifisha imani wakati fulani Visiwani hapo?

Sasa unaweza kujitajirisha mwenyewe!

Mwadhama Polycap Kardinali Pengo,
Mh. Rais wa Zanzibar Ali Mohamed Shein,
Mhashamu Askofu Augustine Shao,
Wahashamu Maaskofu Wakuu,
Wahashamu Maaskofu,
Waheshimiwa Mapadre, Watawa na Taifa la Mungu,

“Hii ndiyo siku aliyoifanya Bwana, Tufurahi na kuishangilia!”

Wapendwa Taifa la Mungu, leo tunayo kila sababu ya kufurahi, kushangilia, na kumshukuru Mungu kwa zawadi ya imani kwa Mungu katika Kanisa, ambayo kwayo leo tunakusanyika hapa. Leo tunaadhimisha kumbukumbu ya miaka 150 ya Ukristo ulioendelevu na wakudumu hapa Zanzibar tuliopokea toka wamisionari walipoingia kwa mara nyingine tena mwaka 1863, safari hii wakitokea Jimbo la St. Denis, Reunion. Hiki ni kipindi endelevu na cha kudumu kwani hapo kabla ukatoliki ulishafika Zanzibar wakati wamisionari kutoka Ureno walipofika hapa mwaka 1498. Ukristo ulidumu kwa karne mbili kabla ya Wamisionari kufukuzwa na Waarabu mnamo mwaka 1698.

Tunakusanyika hapa leo kwa wingi wetu kumshukuru Mungu kwa sababu Jimbo la Zanzibar litabaki kuwa “Jimbo mama yetu wa Imani”, kwa sababu ni kupitia mlango wa Zanzibar imani Katoliki ilitufikia Tanzania Bara na maeneo mengine ya Afrika Mashariki na Kati. Mbegu ile ya imani iliyopandwa Zanzibar imekua na kuwa mti mkubwa unaoendelea kukua na kuzaa matunda ya kudumu katika imani. Kwa hiyo, pamoja na kumshukuru Mungu, tumekuja hapa tena kusali pamoja na kumuomba Mungu atujalie neema na ujasiri wa kuwa Wamisionari imara na jasiri wa “Uinjilishaji wa kina ulio endelevu na wa kudumu”.

Wapendwa Taifa la Mungu; pamoja na furaha tunayokuwa nayo leo, tunatambua pia kuwa Kanisa la Zanzibar, katika ujumla wake, linapita katika kipindi cha misukosuko ya kiimani. Matukio ya hivi karibuni ya mashambulizi ya chinichini na hata ya waziwazi, mauaji ya viongozi wa dini ya kikristo n.k yanachora picha ya kukosekana uhuru wa kuabudu na kuheshimiana. Kwa msisitizo mkubwa, tunapenda kutoa wito kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kulinda na kutetea haki za watu wote katika Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

Tanzania ni nchi yenye watu wenye makabila tofauti, dini tofauti na hata madhehebu tofauti. Hakuna Mtanzania aliyemkimbizi ndani ya Tanzania. Mkristo anayeishi Zanzibar, kama alivyo mtu wa dini nyingine yoyote ana haki sawa kikatiba. Tofauti zetu, ili mradi hatuvunji sheria, ndio utajiri wetu. Utofauti wetu ndio unaotufanya tukamilishane. Hivyo, tunaomba serikali na watu wote wa Zanzibar tuwe waamini wa msingi wa kwanza kabisa wa maisha ya mwanadamu kuwa: “sote ni wana wa Mungu, kabla ya dini zetu, rangi zetu, makabila yetu.” Wito wetu si kwamba tuvumiliane bali tuheshimiane, tupendane na tudumishe umoja wetu.

Wapendwa Taifa la Mungu, tunapenda leo kutoa shukrani zetu na pongezi za dhati kwa Mhashamu Baba Askofu Augustino Shao kwa utume uliotukuka. Tunapenda kukupongeza wewe Baba Askofu, Mapadre, Watawa na Waamini wote kwa ujasiri wenu, moyo wenu wa kujitolea mkimhudumia kila mtu bila kujali dini yake, kabila lake, wala rangi yake.

Huo ndiyo ukristo. Hiyo ndiyo fahari ya imani tunayoitangaza; yaani kuiona sura na mfano wa Mungu katika kila mtu aliyeumbwa na Mungu. Ushuhuda wenu wa imani unatuimarisha sote, hivi kwamba leo tunakuja hapa kusema: “asante sana,” na “tuko pamoja nanyi.”

Wapendwa wanakanisa la Zanzibar, ninyi si kanisa dogo: “Usiseme mimi ni mtoto; kwa sababu kokote nitakako kutuma utakwenda” (Yer 1:7). Hivyo ndivyo Bwana anavyomwimarisha nabii. Ninyi si wadogo. Mama hawezi kuwa mdogo. Ninyi Kanisa la Zanzibar ndiyo mliotumwa kuisambaza imani Afrika Mashariki na Kati na bado mnayo dhima kuwa ya ushuhuda.

Msiogope! Ishuhudieni imani kwa ujasiri! Uwepo wenu Zanzibar si ajali bali ni mapenzi ya Mungu. Mchango wenu katika maendeleo ya Zanzibar katika nyanja za elimu, afya, utamaduni, n.k., ni mkubwa sana. Tunaishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jitihada za kulinda watu wote na Kanisa linazidi kuomba ushirikiano zaidi katika kutimiza majukumu mbalimbali ya kidini pamoja na ya kijamii.

Baba Askofu na wanakanisa wa Zanzibar tunarudia kusema Msiogope! Hilo ni himizo la Kristo Mfufuka aliyeshinda mauti na kifo. Simameni imara katika Imani, simameni imara katika ukristo, simameni imara katika kukuza tunu zetu kama Taifa la Mungu. Amina.








All the contents on this site are copyrighted ©.