Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu za
Rambirambi Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Anne Semamba
Makinda kufuatia kifo cha Mbunge wa Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi
(CCM), Said Ramadhan Bwanamdogo.
Mheshimiwa Said Ramadhan Bwanamdogo amefariki
tarehe 22 Januari, 2014 katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Taasisi ya Mifupa
(MOI) alikokuwa amelazwa akiendelea kupatiwa matibabu.
“Nimeshtushwa, nimesikitishwa
na kuhuzunishwa mno na taarifa za kifo cha Mbunge wa Jimbo la Uchaguzi la Chalinze
kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi, Mheshimiwa Said Ramadhan Bwanamdogo, kilichotokea
tarehe 22 Januari, 2014 akiwa amelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Taasisi
ya Mifupa (MOI) akiendelea na matibabu”, amesema Rais Kikwete akiomboleza kifo cha
Mbunge Bwanamdogo.
“Kwa hakika kifo cha Mbunge huyu ambacho kimenigusa mno,
siyo tu ni pigo kubwa kwa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alikokuwa
akichangia kwa umahiri mijadala na hoja mbalimbali bali pia kwa Wananchi wa Jimbo
la Chalinze ambao alikuwa akiwawakilisha vyema na kwa uhodari mkubwa katika Bunge
hilo”, ameongeza kusema Rais Kikwete kwa masikitiko.
“Kufuatia taarifa za
msiba huu, ninakutumia wewe Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa
Anne Semamba Makinda Salamu zangu za Rambirambi kutoka dhati ya moyo wangu kwa kumpoteza
Mbunge, Said Ramadhan Bwanamdogo”, ameongeza kusema Rais Kikwete katika Salamu zake.
Aidha
Rais Kikwete amemwomba Spika Makinda kumfikishia Salamu zake za Rambirambi na pole
nyingi kwa familia ya Marehemu kwa kupotelewa na Baba, Kiongozi na Mhimili madhubuti
wa familia ambaye kwa hakika alikuwa tegemeo kubwa kwao katika kuiendesha vyema familia
yao. Hata hivyo amesema hawana budi kuutambua ukweli kwamba kazi ya Mungu haina makosa.
Amewahakikishia
Wanafamilia, ndugu na jamaa wa Marehemu Said Ramadhan Bwanamdogo kuwa, katika msiba
huu, hawako peke yao kwani yeye binafsi yuko pamoja nao katika kipindi chote cha maombolezo
na kwamba msiba huu ni wa wote.
Amewaomba Wanafamilia kuwa wavumilivu, watulivu,
wenye subira na ujasiri ili waweze kuhimili machungu ya kuondokewa na Kiongozi na
Mhimili wa familia. Rais Kikwete amesema anamuomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema
aipokee na kuilaza Mahala pema Peponi Roho ya Marehemu Said Ramadhan Bwanamdogo, Amina.