2014-01-22 07:52:06

Licha ya majanga, kinzani na misigano mbali mbali, Nigeria itaendelea kushikamana kama taifa moja!


Mwaka 2014 ni muhimu sana kwa historia ya wananchi wa Nigeria, kwani wanaadhimisha Jubilee ya Miaka 100 ya Umoja wa Kitaifa baada ya kuunganisha Falme za Kaskazini na Kusini na hivyo Nigeria kama inavyojulikana kwa sasa ikaundwa.

Licha ya majanga, kinzani na misigano mbali mbali ya kisiasa, kijamii na kiimani inayoendelea kujitokeza nchini Nigeria, lakini bado Nigeria kama taifa litaendelea kuwepo na kwamba, Mwenyezi Mungu hatawaacha watu wake wagawanyike tena! Dhana hii inapaswa kufanyiwa kazi na wanasiasa kwa kuonesha utashi wa kisiasa unaopania kujenga na kudumisha msingi wa umoja na mshikamano wa kitaifa.

Hayo yamesemwa hivi karibuni na Askofu Josiah Idowu Fearon wa Kanisa Anglikani, Jimbo la Kaduna, nchini Nigeria, wakati huu Nigeria inapojiandaa kuadhimisha kilele cha Jubilee ya Miaka 100 ya Umoja wa Kitaifa sanjari na maandalizi ya uchaguzi mkuu hapo mwakani. Umoja wa Kitaifa nchini Nigeria unajikita katika imani kwa Mungu mmoja ingawa wakati mwingine kuna misigano katika uelewa huu kiasi cha kusababisha mauaji na hata vita vya kidini, dhana ambayo kwa sasa imepitwa na wakati.

Ni matumaini ya Askofu Fearon kwamba, hata baada ya uchaguzi mkuu nchini Nigeria, unaotarajiwa kufanyika mwaka 2015, Wananchi wa Nigeria ambao wengi wao ni Wakristo na Waislam wataendelea bado kushikamana, kwani kuna kikundi cha watu wachache wanaotaka kuivuruga nchi kwa mafao yao binafsi, wakati mwingine kwa kutumia mgongo wa masuala ya kidini, jambo ambalo ni hatari kwa ustawi, umoja na mshikamano wa kitaifa.

Askofu Fearon anawaalika viongozi nchini Nigeria kutoa kipaumbele cha kwanza kwa heshima na utu wa binadamu; maendeleo na mafao ya wengi na kamwe wasitafute nafasi za uongozi kwa ajili ya kujineemesha wao na familia zao. Viongozi wawe mfano wa kuigwa; wanaosimama kidete kulinda na kutetea umoja na mshikamano wa kitaifa; ukweli na uhuru wa wote bila kumezwa na udini pamoja na ukabila mambo ambayo ni sumu ya umoja na mshikamano wa kitafa.

Serikali iwe makini kuwalinda watu na mali zao, ili kudhibiti vitendo vya uhalifu ambavyo vimekuwa ni tishio kwa usalama wa wananchi na mali zao nchini Nigeria, hali ambayo imewafanya baadhi ya wananchi wenye uwezo kukodi walinzi wa kujitegemea.







All the contents on this site are copyrighted ©.