2014-01-20 08:05:11

Uchu wa mali na madaraka visilitumbukize taifa katika vita na majanga!


Baraza la Makanisa Sudan ya Kusini linawataka wahusika wakuu katika vita ya wenyewe kwa wenyewe inayoendelea kusababisha majanga makubwa nchini humo kusitisha mara moja vita hiyo bila masharti na kuendelea kujikita katika majadiliano yanayopania kupata suluhu ya amani na maendeleo ya kweli nchini humo.

Uchu wa madaraka unataka kulitumbukiza taifa katika maafa ambayo yatakwamisha hata kiwango kidogo cha maendeleo kilichoanza kupatikana tangu Sudan ya Kusini ilipoamua kuwa ni nchi huru.

Viongozi wa Baraza la Makanisa Sudan ya Kusini, wanawataka wahusika wote kuondokana na falsafa ya kutumia nguvu kufikia malengo yao ya kisiasa na badala yake wajikite katika majadiliano yanayosimikwa kwenye misingi ya ukweli na uwazi. Kila mwananchi anawajibu wa kulinda na kutetea umoja na mshikamano wa kitaifa ambao umepitia katika magumu. Mwaka 2010, kwa pamoja walijiunga na kupiga kura ya maoni na tarehe 9 Julai 2011 wakasherehekea Uhuru wa Sudan ya Kusini.

Jambo la kusikitisha ni kuona kwamba, baada ya miaka miwili tu ya Uhuru, wananchi wa Sudan ya Kusini wameanza tena vita ya wenyewe kwa wenyewe! Kuna maelfu ya watu ambao wamelazimika kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa mali na maisha yao.

Baraza la Makanisa Sudan ya Kusini katika ujumbe wake linasema: watu wametenda dhambi, wanapaswa kutubu na kumwongokea Mungu, ili waweze kujipatanisha na jirani zao, kama sehemu ya mchakato wa uponyaji. Wananchi wajikite katika amani badala ya kuvumisha mambo yanayowagawa na kuwasambaratisha kama nchi moja. Wanasiasa waendeleze majadiliano ya kweli kwa ajili ya mafao na ustawi wa wananchi wote wa Sudan ya Kusini.

Wananchi wote wasimame kidete kulinda na kutetea zawadi ya maisha, wakate kujitumbukiza katika vita. Watu ambao wamevunja Katiba ya nchi wafikishwe kwenye mkondo wa sheria na kamwe watu wasijichukulie sheria mikononi mwao. Serikali na wapinzani watoe nafasi kwa Mashirika ya Misaada kutoa huduma kwa wananchi na kwamba, umefika wakati wa kujikita katika mchakato wa amani.

Viongozi wa Baraza la Makanisa Sudan ya Kusini wanaipongeza IGAD na Jumuiya ya Kimataifa kwa kuendelea kutoa misaada pamoja na kuhamasisha majadiliano ya kisiasa ili amani ya kweli iweze kupatikana nchini Sudan ya Kusini. Wanayapongeza Makanisa kwa kuendelea kutoa huduma kwa watu wanaohitaji msaada. Wataendelea kuhamasisha amani, ukweli, msamaha na upatanisho, ili kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa. Wanawataka wananchi wasikubali kugawanywa kwa misingi ya kisiasa, kidini wala kikabila. Kila mwananchi awajibike katika kujenga nchi yake na kamwe asiwe ni sababu ya kubomoka na kuporomoka kwa maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa.








All the contents on this site are copyrighted ©.