Halmashauri tumieni nguvu kazi ya vijana katika ujenzi wa nyumba nafuu!
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amezitaka Halmashauri zote 160 za Miji na Wilaya
zilizoko nchini kuhakikisha zinaunda vikundi vya vijana vya ujenzi wa nyumba nafuu
(building brigades) ili viwe sehemu ya miradi ya kila Halmashauri. Ametoa agizo hilo
Jumatatu, Januari 20, 2014 wakati akizungumza na wahitimu wa mafunzo ya wataalam wa
mashine za kutengeneza matofali kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu kwenye
hafla fupi iliyofanyika Mwenge jijini Dar es Salaam.
Mafunzo hayo yaliyoanza
Januari 6 - 17, mwaka huu yaliendeshwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) pamoja
na Mamlaka ya Elimu ya Ufundi Stadi (VETA) kwa kushirikiana na Wakala wa Utafiti wa
Vifaa Bora vya Ujenzi (NHBRA) iliyo chini ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo
ya Makazi. Mafunzo hayo ambayo yanahusu namna ya kutumia mashine za Hydraform ni pamoja
na kutambua udongo unaofaa kutengenezea matofali na namna ya kujenga kwa kutumia matofali
hayo.
Waziri Mkuu alisema alimshawishi Mkurugenzi Mtendaji wa NHC, Bw. Kyando
Mchechu atafute mbinu za kutumia teknolojia rafiki wa mazingira ili kuepuka janga
la uharibifu wa mazingira unaosababishwa na matumizi makubwa ya kuni mbichi ili kuchoma
matofali. “Licha ya kuwa utengenezaji wa matofali ya kuchoma unatekeleza azma ya Serikali
ya kutaka wananchi wake wawe na nyumba bora, kwa kweli roho huwa inaniuma hasa ukizingatia
kiasi kikubwa cha miti inayokatwa kuyachoma hayo matofali hadi yawe imara, tena ikiwa
mibichi,” alisema.
Aliipongeza Wakala wa Utafiti wa Vifaa Bora vya Ujenzi (NHBRA)
kwa kubuni mashine hizo ambazo alisema zinauzwa kwa bei ambayo Halmashauri inaweza
kuzimudu. “Mkurugenzi Mkuu ameniambia kila mashine inauza kwa sh. 450,000/- na inaweza
kutengeneza matofali 700 kwa siku moja… hayo matofali yanatumia mifuko saba tu ya
saruji. Hili ni jambo linalowezekana!” alisisitiza.
“Wakurugenzi wapangeni
vijana wenu katika building brigades ili wanufaike na mapando huu. Na Wakurugenzi
wa Dodoma itabidi tuwapigie kelele ili wawasimamie wananchi waweze kupata nyumba kupitia
mpango huu,” aliongeza. Alisema anataka wachangamkie haraka hizo mashine kwa sababu
zinasaidia uhifadhi wa mazingira, zinachochea ufanisi wa teknolojia, zinapunguza gharama
za ujenzi na zinasaidia kutoa ajira kwa vijana.
“Kila Halmashauri itapewa
mashine nne, na kila mashine inahudumiwa na vijana 10 kwa hiyo itachangia ajira ya
moja kwa moja kwa vija 6,400. Hata hivyo aliwasihi watakaoendesha miradi hiyo wasitoze
bei kubwa kwa matofali watakayotengeneza ili wananchi wengi waweze kumudu bei na wabadili
hadhi za makazi yao,” alisema.
Alimtaka Bw. Mchechu aweke mpango wa kuendeleza
kampeni hiyo kwa miaka mitano mfululizo ili uweze matokeo chanya kwa jamii badala
kuanzisha mwaka na kuachia katikati.
Mapema, Mkurugenzi Mtendaji wa NHC, Bw.
Kyando Mchechu alisema chini ya mpango wa kusaidia miradi ya maendeleo inayofanywa
na jamii (CSR), Shirika lake limekuwa linachangia sekta za afya na elimu na hivi sasa
wamelenga vijana hasa kutoa ajira katika sekta ya ujenzi. “Shirika limegawa mashine
640 za kufyatulia matofali na kila Halmashauri itapatiwa mashine nne, …kwa kuanzia
NHBRA wameahidi kutoa mashine 320 kwa mkupuo mara zitakapokamilika,” alisema.
Aliwasihi
wakuu wa wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri watoe ushirikiano kwa shirika hilo ili
mpango huo wa kutoa jaira kwa Vijana uweze kufanikiwa. Mafunzo hayo yalihusisha wataalamu
50 waili kutoka kila mkoa ambapo kati yao 34 walikuwa ni walimu wa VETA na 16 ni wahitimu
wa VETA. NHC na Tumeelezwa na VETA zimekubaliana ya kuwatumia vijana waliohitimu VETA
kutengeneza matofali katika Kanda Tano zenye miradi ya ujenzi wa nyumba za gharama
nafuu wakitumia mashine za kisasa za Hydraform.