Baraza la Kipapa la Familia kwa kushirikiana na Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki
Italia limeanzisha kampeni ya siku mbili kwa ajili ya kuhamasisha mchakato wa upatikanaji
wa amani nchini Syria. Vita na machafuko ya kisiasa na kijamii yamepelekea maelfu
ya watu kupoteza maisha na mali zao; watu wengi wamekimbia makazi yao kwa kuhofia
usalama wa maisha.
Kutokana na kuguswa na mahangaiko na mateso ya wananchi
wa Syria, Jumamosi na Jumapili kwenye viwanja vya mpira wa miguu nchini Italia, kutaendeshwa
kampeni ya mshikamano wa upendo na wananchi wa Syria. Hayo yamebainishwa na Baraza
la Kipapa la Familia, kama sehemu ya utekelezaji wa changamoto iliyotolewa na Baba
Mtakatifu Francisko alipokuwa anazungumza na Mabalozi pamoja na wawakilishi wa Mashirika
ya Kimataifa mjini Vatican hivi karibuni.
Kampeni hii inaelekeza nguvu zake
kwa ajili ya mkutano wa majadiliano ya amani awamu ya pili nchini Syria unaotarajiwa
kufanyika mjini Geneva, hapo tarehe 22 Januari 2014. Itakumbukwa kwamba, Mwezi Oktoba,
2013, Baraza la Kipapa wakati wa kufunga Mwaka wa Imani kwa Familia Duniani, waliendesha
Kampeni ya mshikamano wa upendo na familia zilizoko nchini Syria.