2014-01-15 08:06:39

Dumisheni tunu msingi za maisha ya ndoa na familia mintarafu Mafundisho ya Kanisa


Askofu Malcolm McMahon wa Jimbo Katoliki la Nottingham, Uingereza katika barua yake ya kichungaji wakati wa Maadhimisho ya Sherehe ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu anasema, changamoto za kuishi tunu msingi za maisha ya ndoa na familia mintarafu Mafundisho ya Kanisa zinapata chimbuko lake kwa Kristo mwenyewe na kwamba, hii ni dhamana nyeti. RealAudioMP3

Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, familia nyingi zinakabiliana na magumu hasa katika mchakato wa kumwilisha upendo wa Mungu katika maisha ya ndoa na familia. Kanisa lina matumaini makubwa katika Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu maalum kwa ajili ya Familia, ili kuonesha ni kwa jinsi gani Kanisa linatoa kipaumbele cha pekee kwa maisha ya ndoa na familia katika maisha na utume wake ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla.

Mama Kanisa anaendelea kuwahimiza wanandoa na familia kujikita katika sala, kwani familia inayosali, itaweza kudumu na kukabiliana na changamoto za maisha kwa pamoja, bila ya kuteteleka, kwani sala ni uti wa mgongo wa maisha ya ndoa na familia. Familia zijenge na kudumisha ari na moyo wa Sala na Ibada: kwa kusali Rozari Takatifu mara kwa mara; kwa kusoma na kutafakari Neno la Mungu kwa pamoja kama Familia.

Mababa wa Kanisa tangu mwanzo wametambua na kuthamini maisha ya ndoa na familia katika maisha na utume wa Kanisa, ndiyo maana Papa Leo wa kumi na tatu akatangaza Maadhimisho ya Siku kuu ya Familia kwa Kanisa zima.

Askofu McmMahon anasema, katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya mawasiliano, ndoa na familia zinakabiliana na changamoto nyingi za maisha, lakini hakuna haja ya kukata wala kukatishwa tamaa kwani Familia takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu inapaswa kuwa ni mfano na kielelezo cha kuigwa na waamini wote.

Familia iwe ni mahali ambapo wanafamilia na majirani wanaonjeshana tone la upendo na msamaha. Hapa ni mahali pa kukumbatia na kuenzi Injili ya Uhai dhidi ya utamaduni wa kifo. Familia iwe ni chemchemi ya upendo na ukarimu kwa watu wanaoteseka kutokana na majanga mbali mbali ya maisha kama vile wakimbizi, wahamiaji na wote waliokumbwa na maafa asilia sehemu mbali mbali za dunia.

Familia iwe ni mahali pa kulinda, kuendeleza na kurithisha tunu bora za maisha ya ndoa na familia, kwa kutambua kwamba, ndoa ni muungano thabiti kati ya Bwana na Bibi na wala si jambo la mpito! Huu ndio uelewa kadiri ya mpango wa uumbaji na ukombozi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya binadamu na kwamba, ndoa ni kielelezo cha upendo wa juu kabisa kwa Kristo na Kanisa lake!

Licha ya magumu na changamoto za maisha ya ndoa na familia, lakini bado kuna wazazi na walezi wanaowapenda na kuwathamini watoto wao katika malezi na makuzi; kwani wanatambua kwamba, familia ni kitovu cha kurithisha imani na tunu msingi za maisha ya Kikristo.

Askofu Malcolm McMahon wa Jimbo Katoliki la Nottingham katika barua yake ya kichungaji anasema, kwamba, Baba Mtakatifu Francisko ameziona changamoto za maisha ya ndoa na familia, ndiyo maana ameitisha Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Ndoa, itakayoadhimishwa mjini Vatican Mwezi Oktoba, 2014.

Maswali dodoso yaliyotolewa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Familia yanalenga kujenga na kuimarisha majadiliano kati ya Kanisa la Waamini katika masuala ya ndoa na familia, ili hatimaye, Kanisa liweze kuibua mbinu mkakati wa kichungaji utakaosaidia familia kutekeleza dhamana na wajibu wake ndani ya Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.