2014-01-15 07:49:10

Angola kwa mara ya kwanza inatarajia kuadhimisha Siku ya Vijana Kitaifa 2015


Baraza la Maaskofu Katoliki Angola, linatarajia kunako Mwaka 2015 kuadhimisha kwa mara ya kwanza Siku ya Vijana Kitaifa. Lengo ni kuhakikisha kwamba, vijana kutoka nchini Angola wanapewa nafasi ya kuweza kushirikisha karama na vipaji vyao kwa ajili ya ujenzi, ustawi na maendeleo ya Kanisa na Taifa katika ujumla wake. Hayo yamejadiliwa hivi karibuni katika Bunge la Vijana wa Angola. RealAudioMP3

Askofu Zeferino Martins, Mwenyekiti wa Tume ya Vijana ya Baraza la Maaskofu Katoliki Angola anasema, vijana wengi nchini humo wanakabiliwa na tatizo la ulevi wa kupindukia, hali ambayo inabomoa misingi bora ya maisha ya kikristo na kiutu, kiasi hata cha kudhohofisha maisha ya ndoa na familia. Baraza la Maaskofu Katoliki Angola linasema, kuna haja kwa wadau mbali mbali kuwekeza katika majiundo makini ya vijana, ili kudhibiti tabia ya ulevi ambayo inawatumbukiza vijana hata katika majanga mengine ya maisha.

Maaskofu wanasema, umefika wakati kwa Angola kutoa kipaumbele cha kwanza katika maisha na utume wa Familia. Changamoto hii inakwenda sanjari na maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu Familia itakayoadhimishwa mjini Vatican mwezi Oktoba, 2014.








All the contents on this site are copyrighted ©.