2014-01-14 09:43:55

Vita kamwe haiwezi kuwa ni njia ya amani!


Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini ndiye aliyeongoza Warsha ya Siku moja iliyokuwa imeandaliwa na Baraza la Kipapa la Sayansi Jamii kuhusu hali tete nchini Syria kutokana na maelfu ya watu wanaoendelea kupoteza maisha yao na wengine kulazimika kuyakimbia makazi yao.

Wajumbe wa warsha hii, wanasema, kuna haja kwa wadau mbali mbali kuanzisha mchakato wa upatanisho na ujenzi mpya wa Syria unaosimikwa katika haki na amani. Wahusika wakuu katika mgogoro huu waoneshe utashi wa kisiasa wa kutaka kumaliza mgogoro huu kwa njia ya amani. Nchi za nje ambazo zimekuwa zikiendelea kufanya biashara ya silaha nchini Syria zinapaswa kusitisha mara moja, ili kuokoa maisha ya watu na kama sehemu ya kwanza ya mchakato wa upatanisho.

Baada ya kusitisha mapigano, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuanza juhudi za ujenzi mpya wa Syria kwa kuwasaidia wakimbizi na wahamiaji kupata mahitaji msingi, tayari kushiriki katika ujenzi wa nchi yao. Ujenzi huu unaweza kuanza tu, ikiwa kama masuala ya kisiasa na kijamii yatakuwa yamepatia ufumbuzi wa kudumu. Vijana na maskini wapewe kipaumbele cha kwanza, ili kuwawezesha kupata ajira sanjari na kuchangia kwa hali na mali katika ujenzi mpya wa Syria.

Wananchi wa Syria hawana budi kuanza kujielekeza wenyewe katika majadiliano ya kina yanayosimikwa katika ukweli na uwazi; upendo na mshikamano wa kitaifa, ili kuendeleza dhana ya upatanisho wa kitaifa unaopania pamoja na mambo mengine kufukia chuki na uhasama uliojitokeza katika siku za hivi karibuni, ili watu waanze tena kuaminiana na kusaidiana kwa hali na mali kama ndugu.

Jumuiya ya Kimataifa inatambua kwamba, ukosefu wa amani na utulivu nchini Syria unaweza kusababisha athari kubwa katika eneo la Mashariki ya Kati. Kuna mataifa makubwa ambayo yanaendelea kujiimarisha huko Syria kwa sababu za kiuchumi. Amani na usalama ni mambo yanayowezekana nchini Syria kwani historia inaonesha kwamba, wananchi wa Syria kwa miaka mingi waliweza kuishi kwa amani na utulivu na kwa sasa wanaweza pia kuanza kufanya hivyo.

Wajumbe wa Warsha kwa ajili ya Syria wanasema, Awamu ya Pili ya Mkutano wa Syria huko Geneva ujitahidi kuwashirikisha wadau wote ndani na nje ya Syria yenyewe kwa kuzingatia pia makubaliano yalihyofikiwa kati ya Irani na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa pamoja na Ujerumani kuhusiana na masuala ya Kinyuklia, ili kujenga na kuimarisha hali ya kuaminiana na kushirikiana, ili hatimaye, kupata amani ya kudumu nchini Syria. Majadiliano kati ya Israeli na Palestina hayana budi kusonga mbele kwa kusaidiwa na Marekani ambayo imekuwa ni mshiriki mkubwa.

Wajumbe wa warsha hii iliyofanyika katika faragha wanasema, amani ya kudumu inasimikwa katika msingi wa utashi wa kisiasa wa kusitisha mapigano; kuanza majadiliano ya kweli kwa kuwashirikisha wadau mbali mbali. Awamu ya Pili ya mkutano wa Syria huko Geneva uwe ni msingi wa amani ya kudumu na mwanzo wa mabadiliko ya kisiasa na kijamii nchini Syria. Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kukumbusha kwamba, vita kamwe haiwezi kuwa ni njia ya amani. Wananchi washinde ubinafsi kwa kuongozwa na dhamiri nyofu kutafuta mafao ya wengi kwa njia ya majadiliano na upatanisho; ili kudumisha amani na maridhiano.







All the contents on this site are copyrighted ©.