Tanzania yaomba msaada kutoka China kuhusu mipangomiji!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete ameiomba Jamhuri ya
Watu wa China kusaidia mipangomiji katika baadhi ya maeneo ya kimkakati ya Tanzania
na China imekubali kuleta timu ya wataalam kufanya tathmini katika maeneo hayo yote
ama baadhi ya maeneo hayo ili kujua mahitaji kamili ya mipangomiji ya maeneo hayo.
Rais
Kikwete alitoa ombi hilo Jumapili, Januari 12, 2014, wakati alipokutana na kufanya
mazungumzo na Waziri wa Nyumba, Makazi na Maendeleo ya Mjini na Vijiji wa China,
Mheshimiwa Jiang Weixin, mazungumzo yaliyofanyika Ikulu, Zanzibar. Rais Kikwete alikuwa
katika ziara ya kikazi ya siku tatu Tanzania Visiwani ambako jana alishiriki katika
Sherehe za Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar wakati Mheshimiwa Weixin alimwakilisha
Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Mheshimiwa Xi Jinping katika sherehe hizo.
Katika
mazungumzo hayo, Rais Kikwete alimweleza Mheshimiwa Weixin kuhusu juhudi zinazofanywa
na Serikali kuhusu umuhimu wa upangaji miji na kuiweka miji ya Tanzania katika hali
nzuri akisisitiza kuwa Serikali inakabiliwa na changamoto za ukosefu wa uwezo wa kiufundi,
ukosefu wa vifaa na ukosefu wa uwezo wa kifedha ili kuifanya kazi hiyo kwa ufanisi..
Rais
Kikwete amesema kuwa pamoja na kwamba changamoto za mipangomiji ziko katika miji yote
ya Tanzania, ikiwamo Dar Es Salaam, lakini Serikali kwa sasa inapenda kuelekeza nguvu
zake katika miji mitatu ambayo ina uwezo mkubwa wa kuendelea kwa kasi kubwa zaidi
katika miaka michache ijayo na hivyo lazima iendelee ikiwa imepangwa vizuri.
Rais
Kikwete ameitaja miji hiyo mitatu kuwa ni mji mpya wa Kigamboni, Dar es Salaam na
miji ya Mtwara na Lindi ambayo kwa sababu ya uvumbuzi wa gesi na uchumi utakaotokana
na uvumbuzi huo, inayo uwezo mkubwa wa kupanuka na kukua kwa haraka na isipopagiliwa
vizuri kutokea mwanzo inaweza kuishia ikipanuka kwa ujenzi holela.
“Chukulia
mfano wa Jiji la Dar es Salaam Mheshimiwa Waziri. Mamilioni ya watu wanaishi katika
jiji hili lakini asilimia 70 ya mji huu haikupimwa na imejengwa holela tu. Ni asilimia
30 ya Dar es Salaam iliyopimwa. Hatuwezi kuiruhusu miji mingine, hasa ya kimkakati,
kupanua na kukua kwa namna hii.”
Baada ya kumsikiliza Rais Kikwete, Waziri
Weixin alisema kuwa ameelewa changamoto zinazoikabili Tanzania na kuwa Wizara yake
itatuma wataalam wake kuja Tanzania kufanya tathmini katika maeneo muhimu kwa kushirikiana
na wataalam wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambayo Waziri wake,
Anna Tibaijuka alihudhuria mazungumzo hayo.
Rais Kikwete na Waziri Weixin pia
walizungumzia hali ya uhusiano kati ya nchi na wananchi wa nchi hizo mbili ambao utafikisha
miaka 50, Mei, mwaka huu, 2014, kufuatia kuanzishwa kwa uhusiano wa kibalozi kati
ya nchi hizo mwaka 1964. “Tanzania imenufaika sana na uhusiano huu katika miaka 50
ilitopita. China imeisaidia sana katika miaka 50 hiyo. Tunahitaji kuuendeleza uhusiano
huu na bado tunahitaji kuendelea kuungwa mkono na China kwa sababu pamoja na yote,
Tanzania bado ni nchi inayoendelea.”