2014-01-14 11:15:41

Kinzani za kijeshi nchini Msumbiji zinaweza kusababisha maafa makubwa!


Wasi wasi wa kuvunjika kwa amani unaendelea kuongezeka nchini Msumbiji kutokana na kinzani zinazojitokeza kati ya Jeshi la Serikali linaloongozwa na Chama cha FRELIMO na Jeshi la Waasi kutoka Chama cha upinzani cha RENAMO. Mapigano ya hivi karibuni kati ya Jeshi la Serikali na Renamo, wilayani Homoime, Jimbo la Inhambane yamepelekea watu kadhaa kupoteza maisha.

Mashambulizi ya kijeshi yaliyofanywa na Jeshi la Serikali ya Msumbiji kwenye Makao makuu ya RENAMO, mwanzoni mwa Mwezi Oktoba, 2013 yalisababisha uhusiano kati ya RENAMO na FRELIMO kusuasua kwa kiasi kikubwa na hapo ukawa ni mwanzo wa kutoweka kwa amani nchini Msumbiji. Inasikitisha kuona kwamba, vita ya wenyewe kwa wenye iliyodumu nchini Msumbiji tangu Mwaka 1975 hadi Mwaka 1992 inataka kuzuka tena.

RENAMO inataka kuundwa kwa Tume huru ya uchaguzi nchini Msumbiji pamoja na kuwa na usawa katika ugavi na matumizi ya rasilimali za nchi kuliko hali ilivyo kwa sasa kwani inasemekana kwamba, wanaofaidi zaidi ni viongozi wa Serikali iliyoko madarakani wanaotumia nyadhifa zao kuwanyanyasa viongozi wa vyama vya upinzani.







All the contents on this site are copyrighted ©.