2014-01-11 09:03:50

Rutubisheni utu wenu kwa njia ya imani bila ya kuichafua kwa kukumbatia malimwengu!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa, tarehe 10 Januari 2014 amekutana, amezungumza na kuwashukuru wafanyakazi walei wanaotoa huduma ya kutukuka mjini Vatican, katika mapokezi ya viongozi mbali mbali wanaofika mjini Vatican kumtembelea Khalifa wa Mtakatifu Petro pamoja na kumsindikiza Baba Mtakatifu wakati wa shughuli zake za kitume kwenye Uwanja au Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.

Baba Mtakatifu anasema huduma yao ni muhimu sana kwa watu mbali mbali wanaofika mjini Vatican ili kukutana na kuzungumza na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Wao kimsingi ni kioo cha maisha na utume wa Kanisa mjini Vatican, jambo linalohitaji, uungwana na ukarimu kwa wageni. Maisha ya kiutu hayana budi kurutubishwa na imani inayotolewa ushuhuda bila kuichafua kwa kutaka kukumbatia malimwengu.

Baba Mtakatifu anasema, Kanisa linahitimisha Kipindi cha Noeli, kilichowapatia waamini fursa ya kumtafakari Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, akazaliwa mjini Bethelehemu, kielelezo cha upendo wa Mungu kwa binadamu. Mwanga ulioletwa kwa kuzaliwa kwa Yesu Kristo uwe ni sehemu ya ushuhuda wa maisha ya waamini katika uhalisia wa maisha yao ya kila siku: ndani ya familia na sehemu zao za kazi. Furaha ya imani ijioneshe kwa namna ya pekee katika upendo, ukarimu pamoja na kuwajali wengine.

Baba Mtakatifu amehitimisha hotuba yake kwa kuwaweka wafanyakazi hao walei pamoja na familia zao chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria, ili aweze kuwasindikiza na kuwalinda katika hija ya maisha yao hapa duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.