2014-01-11 14:59:08

Mwaka wa shughuli za Mahakama kuu ya Vatican wafunguliwa rasmi!


Kardinali Raymond Leo Burke, Mwenyekiti wa Mahakama kuu ya Vatican, Jumamosi, tarehe 11 Januari 2014 ameufungua Mwaka wa 85 wa shughuli za Mahakama kuu ya Vatican kwa Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.

Kwa upande wake, Professa Gian Piero Milano, Mhamasishaji wa amani Mahakama kuu ya Vatican anasema kwamba, wao wanatekeleza shughuli zao kwa kuzingatia utu na heshima ya binadamu. Wanapania kujenga na kuimarisha upendo, udugu na mshikamano kati ya watu pamoja na kusimama kidete kulinda na kutetea haki kwa kuzingatia ukweli, upendo, ili kuchangia ustawi na maendeleo ya wengi mintarafu uwezo na fursa za kila mtu. Yote haya yanalenga ujenzi wa amani ya kweli kati ya watu.

Hotuba ya ufunguzi kuhusu shughuli za Mahakama kuu ya Vatican imegusia kwa namna ya pekee kuhusu: vyanzo vya sheria za Mahakama za Vatican, Marekebisho ya Sheria yaliyofanywa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI; sheria zinazotekelezwa chini ya uongozi wa Papa Francisko pamoja na baadhi ya marekebisho ya taratibu na sheria za makosa ya jinai.

Jambo kubwa zaidi ni sheria za udhibiti wa utakatishaji wa fedha haramu kwa ajili ya kugharimia vitendo vya kigaidi pamoja na ushirikiano wa vyombo mbali mbali mjini Vatican katika utekelezaji wa sheria za makosa ya jinai. Amefafanua kwa kina na mapana, shughuli za Mahakama kuu ya Vatican zilizotekelezwa katika Mwaka wa Mahakama 2012 - 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.