2014-01-11 15:00:53

Askofu Abou Khazen ni mapambazuko ya matumaini huko Mashariki ya Kati, ili kujenga na kuimarisha haki na amani dhidi ya chuki na vita!


Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki, Jumamosi, tarehe 11 Januari 2014, amemweka wakfu Askofu Georges Abou Khazen wa Jimbo la Kitume la Aleppo, lililoko nchini Lebanon. Katika mahubiri yake, amekumbusha umuhimu wa amani ya kweli ambayo kwa sasa ni kilio kikuu cha Jumuiya ya Kimataifa. Kardinali Sandri amewakumbuka wote wanaoendelea kuteseka nchini Syria kutokana na vita ya wenyewe kwa wenyewe ambayo inaendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao.

Kardinali Sandri amewakumbuka na kuwaombea Askofu Boulos Al - Yazigi wa Kanisa la Kiorthodox la Kigiriki pamoja na Askofu Youhanna Ibrahim wa Kanisa la Kiorthodox la Syria, ambao walitekwa nyara Aprili, 2013 hadi sasa hawajulikani mahali waliko. Hili ni giza na uvuli wa mauti unaondelea kutanda katika uso wa dunia.

Ni matumaini ya Kardinali Sandri kwamba, Jumuiya ya Wakristo huko Mashariki ya Kati, itafanikiwa siku moja kuona mwanga unaofungua njia za kiutu, ili kupambana fika na umaskini pamoja na mahangaiko ya watu, kwani Mwenyezi Mungu kamwe hawezi kuwaacha watu wake, bali anatembea nao hatua kwa hatua.

Kuwekwa wakfu kwa Askofu Abou Khazen, yawe ni mapambazuko ya matumaini kwa Syria, kipindi cha ujenzi wa misingi ya haki na amani; dhidi chuki na uhasama, ili watu waonje furaha na utulivu wa ndani, badala ya kuendelea kuelemewa na majonzi na simanzi mioyoni mwao!

Kardinali Sandri anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kusali kwa ajili ya kuombea amani nchini Syria; ili watu waweze kujikita katika mchakato unaopania kujenga na kuimarisha haki, amani na upatanisho wa kitaifa.

Ibada hii imehudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Kanisa kutoka ndani na nje ya Lebanon. Kardinali Sandri ametoa baraka na mshikamano wa dhati kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya wananchi wanaoishi huko Mashariki ya Kati. Kardinali Sandri anatarajiwa kuhitimisha hija yake ya kichungaji nchini Lebanon, Jumatatu, tarehe 13 Januari 2014 kwa kukutana na kuzungumza na Jumuiya ya Chuo Kikuu cha Beirut kinachomilikiwa na kuongozwa na Shirika la Anthony wa Meroniti.







All the contents on this site are copyrighted ©.