Tafakari ya Neno la Mungu, Sherehe za Ubatizo wa Bwana
Mpendwa mwana wa Mungu, tuko tena pamoja katika ile habari ya furaha ndiyo kushirikishana
mapendo ya Mungu kwa njia ya meza ya Neno lake.
Leo ndipo
tunahitimisha kipindi cha Noeli kwa Sikukuu ya Ubatizo wa Bwana na tunaanza kipindi
cha kawaida cha mwaka wa Kanisa. Kumbe leo pia ni Dominika ya kwanza ya kipindi cha
kawaida cha mwaka wa Kanisa.
Katika somo la kwanza Nabii Isaya anatupeni habari
juu ya mtumishi wa Mungu ambaye anapokea Roho wa Mungu na kazi yake itakuwa kuwahukumu
mataifa kwa haki. Ni nuru na mwanga kwa mataifa. Sifa yake nyingine ni mtulivu na
mnyenyekevu na hakati tamaa kwa maana mkono wa Mungu uko juu yake. Mtumishi huyu anakabidhiwa
Roho wa Mungu kwa sababu ya kazi ya Kimungu ambayo ni kujenga amani na kuunganisha
vilivyovunjika.
Kadiri ya Injili ya Luka 4: 18-19 mtumishi huyu ni Yesu Kristo
Masiha aliye Mwana wa Mungu. Anakuja kwa ajili ya kutangaza mwaka wa Bwana ambapo
wafungwa na vipofu wataondolewa katika shida zao. Kristo amekwisha fika kwetu, kazi
yetu sasa ni kupokea ujumbe wake. Namna ya kupokea ujumbe ni kuitika kwanza ule mpango
wa Yohane Mbatizaji na Isaya wa kutengeneza njia ya Bwana, kuondoa visiki na mabonde.
Ndiyo kusema, tunapaswa kufanya hivyo kwa sababu tunasikia kuwa huyu ajaye hatumii
nguvu bali upendo na hivi anahitaji ushirikiano. Kwa jinsi hiyo ni kuweka ubatizo
wetu katika matendo kwa makusudi mazima kabisa.
Mtume Petro akielewa vema nia
na mpango wa Mungu anasimama kama tusomavyo katika kitabu cha Matendo ya Mitume na
kusema, hakika Mungu hana upendeleo, cha msingi ni kufanya bidii ya kumcha Bwana.
Oneni jinsi ambavyo Neno la Mungu linavyopiga kasi, anasema Mtume Petro, si tu kwa
Wayahudi bali kwa ajili ya watu wote. Hata hivyo kwa nini fundisho hili?, Ni kwa sababu
kulikuwa na upinzani dhidi ya ubatizo wa wapagani. Kumbe, Mtume Petro anasema, Kristo
mpakwa mafuta wa Bwana amepiga kazi ya kichungaji baada ya kutiwa mafuta na Roho wa
Bwana bila kubagua. Ni fundisho kwetu kujiimarisha katika utume na kuimarisha umoja
kamili na watu wote milki ya Mungu. Toeni bure kwa maana mmepewa bure. Mpendwa
mwana wa Mungu, daima tangu mwanzo wa Kanisa mpaka leo kumekuwepo maswali juu ya kwa
nini Yesu alibatizwa! Sisi waamini wakristu tunao wajibu wa kujibu maswali haya kwa
upole na unyenyekevu kwa wale wanaotuuliza tukitumainia daima msaada wake katika kutoa
majibu hayo. Ili kuweza kujibu vema maswali hayo yatupasa kutambua yakuwa, kuna tofauti
kati ya ubatizo alioutoa Yohane Mbatizaji na ubatizo wa Kikristo.
Ubatizo
wa Yohane unaitwa ubatizo wa toba, ambao ulikuwa ukifanyika hata katika vijidhehebu
vingine. Ni kwamba watu walikuwa wakizamishwa katika maji na maana yake mmoja aliacha
maisha ya zamani ambayo yalichukuliwa na mkondo wa maji! Ilikuwa ndiyo njia ya kuwaingiza
katika kundi lake Yohane na tena ilikuwa kwa hiari katika mantiki ya kutaka kujiandaa
kwa ajili ya kumpokea Masiha. Hitaji muhimu ili mmoja aweze kubatizwa ilikuwa ni lazima
akubali kukiri hali yake ya dhambi. Kwa mantiki hiyo ndiyo maana Mafarisayo na Masadukayo
walikataa kubatizwa na Yohane Mt. 11:27-33.
Mpendwa, kama hivi ndivyo basi
lazima mmoja aulize swali kwa nini Masiha aombe kubatizwa? Je, jambo hili si kumfanya
Bwana awe chini ya Yohane Mbatizaji? Kwa hakika Masiha hakuwa na haja ya kukiri dhambi
kwa sababu hakuwa nazo na pia hakuwa na haja ya kubadilisha maisha yake maana Kristu
ni yuleyule jana leo na daima! Kutanzua fumbo hilo yafaa kuangalia vema Injili ya
Matayo 3: 13-15. Katika sehemu hii tunakutana na majadiliano kati ya Bwana na Yohane
Mbatizaji. Yohane anakataa kwanza kumbatiza Masiha akisema wewe unakuja kwangu? Mimi
hasa ndiye ninayehitaji kubatizwa nawe na Masiha anasisitiza abatizwe na Yohane akisema
acha iwe hivyo kwa sasa maana ndivyo inavyofaa tuyatekeleze yale yote Mungu anayotaka.
Hapo Yohane akakubali.
Basi mpendwa msikilizaji, Bwana anatambua kuwa hahitaji
ubatizo lakini anataka mwanzoni mwa maisha yake ya hadharani, yaani maisha ya kichungaji
awe upande wa wenye dhambi kama alivyoshiriki mwili wa mtumwa na akashiriki taabu
za ukimbizi akiwa mtoto mdogo huko Misri. Anataka akae nao na kusafiri pamoja nao
wakielekea kileleni, ndio uhuru ambao aliutangaza katika Injili ya Lk 4:18. Toka tendo
hilo takatifu na la kicho. Je, wewe mpendwa msikilizaji wajifunza nini? Mimi pamoja
nawe nataka kugeuza maisha yangu katika jumuiya yawe ni maisha ya kukaa na wadhambi
pasipo kutenda dhambi ili polepole waonje upendo na kubadilika. Ndiyo kusema hukumu
na malumbano yasiyo haki dhidi ya wadhambi havifai kadiri ya fundisho la Bwana. Ninyi
wachungaji yafaa kuwasaidia wenye shida mbalimbali katika parokia ili wafikie kilele
cha uhuru wa wana wa Mungu.
Mpendwa msikilizaji, tukisoma katika Injili ya
Mtakatifu Marko 1:7-11tunapata fundisho la unyenyekevu wa Yohane Mbatizaji na unyenyekevu
wa Kristo. Yohane Mbatizaji anakiri udogo wake ambao ni wa chini kabisa. Maana hata
kushindwa kushika gidamu ya viatu vya Yesu Kristo. Anatufundisha moja kwa moja kuwa
safari ya kumpenda Mungu yatudai kushuka mpaka sakafuni. Mkombozi mwenyewe ndiye pia
kielelezo hasa cha hali ya juu kuhusu unyenyekevu. Anajishusha kwanza na anakuwa mtu,
kana kwamba hiyo haitoshi anaamua kubatizwa wakati hana doa la dhambi. Anatufundisha
kujishusha kukaa pamoja na wadhambi, maana tunabatizwa ili kuokolewa katika uvuli
wa dhambi ya asili kwanza na kuweza kupokea neema za Mungu.
Bwana anapobatizwa
yafaa tuangalie mambo yaliyotokea. Jambo la kwanza ni kupasuka kwa mbingu, ambalo
linatupa habari ileile ya Nabii Isaya katika Dominika za majilio. Nabii anauliza mbona
umetufanya tukose kukutii? Mbona umetuacha hata tukasahau kukucha wewe Bwana? Is.
63:15-19. Isaya anauliza haya maswali kwa maana ni kama hakuna upatano kati ya mbingu
na nchi. Sasa tendo la kupasuka kwa mbingu ni ishara ya mapatano kati ya mbingu na
nchi na mpatanishi ni Kristu katika uwezo wa Utatu Mtakatifu.
Jambo la pili
ni alama ya njiwa, yatukumbusha kile kilichotokea wakati wa mafuriko ya Noa. Wakati
huo mbingu na dunia vilifungwa na njiwa alipotokea akiwa na tawi la mzeituni ilimaanisha
kuwa amani imerejeshwa. Ndiyo kusema kwa ishara ya njiwa kuna amani, ni Roho Mtakatifu
afanyaye kazi katika Yesu Kristu chanzo cha amani. Pili njiwa katika Agano la Kale
alimaanisha nguvu waliyopewa manabii, kwa alama hiyo tunapata kutambua kwa wazi kabisa
kuwa Kristu ana nguvu ya kutenda kazi ya Mungu. Sauti kutoka juu yamaanisha kuwa Kristu
ni wa juu na pia Mungu anaongea na watu wake kwa njia ya Mwanae mpenzi.
Tukumbuke
pia jambo jingine nalo ni lile la Joshua anapowavusha wana wa Israeli pale Jordani,
anapovuka mto anapokea roho wa Mungu ili apate nguvu ya kuwafikisha salama katika
nchi ya ahadi. Ni katika mantiki hiyohiyo Masiha anapotoka majini Roho wa Mungu anashuka
juu yake ili awaongoze wana wa Mungu katika uhuru na kweli ili wafike mbinguni. Watu
wanaoongozwa na Bwana kuelekea kwenye uhuru na kweli ndo sisi, wajibu wetu ni kusikia
sauti ya huyo mchungaji mwema. (Yn. 10).
Mpendwa, ninakutakieni heri na baraka
tele katika sikukuu ya Ubatizo wa Bwana na nakuomba usisahau wajibu wako ulioupokea
kwa njia ya ubatizo, na kwa namna hiyo utakuwa unasherehekea pia ubatizo wako kila
siku ya maisha yako. Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard
Tiganya C.PP.S.