2014-01-10 11:15:22

Balozi wa Vatican nchini Gambia awasilisha hati za utambulisho


Askofu mkuu Miroslaw Adamczyk, Balozi wa Vatican nchini Gambia, hivi karibuni aliwasili nchini Gambia tayari kuanza utume wake. Amepokelewa kwa mikono miwili na viongozi wa Kanisa na Serikali.

Tarehe 5 Novemba, 2013 Askofu mkuu Adamczyk alikutana na Waziri wa Mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa Kimataifa nchini Gambia Dr. Aboubakar A. Senghore na baadaye kuwasilisha hati zake za utambulisho kwa Rais Alhaj Dr. Yahaya A. J. J. Jameh.

Rais amelipongeza Kanisa Katoliki nchini Gambia kutokana na mchango wake wa hali na mali katika maendeleo na ustawi wa wananchi wa Gambia, hususan katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Anasema kuna idadi kubwa ya wananchi wa Gambia ambao wamepata elimu yao kutoka katika shule na taasisi zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki, bila ubaguzi wowote wa kidini.

Rais Jameh, ameelezea kurishwa kwake na uhuru wa kidini nchini Gambia na kwamba, haya ni kati ya mambo Serikali yake inayapatia kipaimbele cha kwanza, kama sehemu ya mchakato wa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na utulivu, chachu makini katika harakati za wananchi kujiletea maendeleo yao wenyewe!

Rais Jameh amemwomba Askofu mkuu Miroslaw Adamczyk, kumfikishia salam zake binafsi na zile za wananchi wa Gambia, heri na matashi mema kwa Noeli na Mwaka Mpya 2014 Baba Mtakatifu Francisko.

Askofu mkuu Adamczyk amewashukuru wote na kuwapatia kheri na baraka kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko na kwamba, anawakumbuka katika sala na sadaka yake. Kanisa linawapongeza wananchi wa Gambia kwa kukuza na kudumisha misingi ya amani, utulivu na kuvumiliana.

Tarehe 3 Novemba 2013, Askofu mkuu Adamczyk aliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Theresa na kutambulishwa kwa Familia ya Mungu nchini Gambia, kazi iliyofanywa na Askofu wa Jimbo Katoliki la Banjul. Baadaye, Askofu mkuu Adamczyk alipata fursa ya kutembelea taasisi mbali mbali zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki nchini Gambia pamoja na kukutana na wawakilishi wa Halmashauri ya Walei, Mapadre na watawa kutoka Jimbo Katoliki Banjul.

Askofu mkuu Miroslaw Adamczyk, Balozi wa Vatican nchini Gambia, alipata nafasi pia ya kuadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu kwenye Seminari ndogo ya Mtakatifu Petro, ambako kuna Waseminari wadogo kumi na wawili wanaoendelea na majiundo yao ya Kikasisi. Hapa inaonekana kwamba, kuna ukame wa miito, changamoto na mwaliko kwa waamini kusali ili kumwomba Bwana wa mavuno aweze kupeleka watenda kazi wema na watakatifu katika shamba lake!







All the contents on this site are copyrighted ©.