2014-01-09 09:07:48

Wananchi wamechoka na vita Sudan ya Kusini!


Viongozi wa kidini na wananchi wa Sudan ya Kusini katika ujumla wao wanasema wamechoka na vita, wanataka kuona: usalama, amani na utulivu vikirejea tena Kusini mwa Sudan ili watu waanza kuchakarika kujitafutia maendeleo! Falsafa ya vita kama suluhu ya migogoro ya kisiasa haina mantiki wala mashiko kwa wananchi wa Sudan ya Kusini. Hivi ndivyo wanavyosema viongozi wa kidini katika tamko lao lililochapishwa kwenye gazeti la "Sudan Tribune".

Tangu machafuko ya kisiasa yajitokeze nchini humo hapo tarehe 15 Desemba 2013, zaidi ya watu 1,000 wamekwisha kufariki dunia na wengine 200, 000 hawana makazi maalum baada ya kuzikimbia nyumba zao kwa kuhofia usalama wa maisha yao.

Wananchi wanataka amani hivyo wanawaomba wadau mbali mbali wanaosaidia kusuluhisha mgogoro huu kuhakikisha kwamba, pande zote mbili zinaweka silaha chini na kuanza mazungumzo na wala machafuko haya ya kisiasa yasigeuzwe kuwa ni sababu ya kuibuka tena vita vya kikabila nchini Sudan ya Kusini.

Wananchi wahamasishwe kushinda kishawishi cha vita vya kikabila kwani huu ni mgogoro wa kugombania madaraka ya kisiasa, unaotaka kulitumbukiza taifa katika maafa makubwa! Mazungumzo kati ya pande zinazohusika yanaendelea mjini Addis Ababa, Ethiopia.







All the contents on this site are copyrighted ©.