2014-01-09 15:19:25

Upendo wa Kikristu si maigizo lakini ni ukarimu na wema halisi


Upendo wa Kikristo daima ni tabia yenye asili ya ukarimu na wema katika maisha ya kila siku. Hivyo, ni upendo unaotenda zaidi kuliko maneno, ni zaidi katika kutoa kuliko kupokea. Ni ujumbe wa Papa Francisko,katika homilia yake wakati wa Ibada ya Misa Alhamis hii asubuhi, Ibada aliyo iongoza katika kanisa dogo la Mtakatifu Marta, Vatican.
Papa amesisitiza, hivyo upendo huo si mahaba ya juu juu lakini ni upendo wa kina usio na choyo katika kutoa na kuwapokea wengine. Ni upendo wa mtu aliye maskini lakini bado ana hamu ya kutaka kutoa hata kidogo alicho nacho kuliko yeye kupokea, na hana la zaidi isipokuwa ni upendo wake kwa Kristo.
Papa Francisko alitoa mafundisho akitafakari barua ya kwanza ya Mtume Yohane , ambamo anasisitiza na kurudia mara kwa mara, iwapo sisi tutapendana kati yetu, Mungu atabaki kuwa nasi na Upendo wake mkalimilifu utakaa ndani mwetu. Papa ametaja uzoefu huu wa imani, umo hasa katika nguzo mbili.

Nazo ni Sisi kuwa ndani ya Mungu na Mungu kukaa ndani mwetu. Hayo ndiyo Maisha ya Mkristu . Na hivyo si kukaa katika roho wa malimwengu , wala kukaa katika purukushani za maisha , wala kukaa katika ibada ya sanamu , wala kukaa katika ubatili, lakini ni kukaa katika Bwana. Naye huungana nasi na kubaki ndani mwetu. Lakini kuna sharti kwamba ni lazima kwanza sisi kukubali kubaki ndani mwake ili nae aweze kubaki ndani mwetu . Bahati mbaya, mara kwa mara sisi binadamu tunapenda kwenda mbali nae, tunashindwa kubaki ndani mwake.

Papa aliendelea kuweka wazi tabia na mienendo ya roho wa upendo wa Kikristo, katika hali ya ubinadamu, kwamba, kukaa katika upendo wa Mungu si tu huustarehesha moyo , lakini pia ni jambo jema kulisikia na kuliishi.

Upendo wa Kikristo daima una thamani ya hali ya juu na ni halisi. Upendo wa Kikristo ni ukweli. Yesu mwenyewe , wakati anazungumzia upendo, hakueleza tu kwa maneno lakini alitenda, aliwalisha wenye wenye njaa , kutembelea wagonjwa n.k, hivyo ni Upendo wa kweli. Na asiyekuwa na upendo huu, humezwa na ubinafsi , siku zote akitafuta kupata faida zake mwenyewe , humezwa na roho wa kutoridhika, na kuonekana tofauti na mwenye upendo wa Kristu ambaye hukaa na moyo wazi, katika kumtumainia Mungu na Mungu huungana katika moyo huo kwa upendo wake Mkamilifu.








All the contents on this site are copyrighted ©.