2014-01-09 10:52:32

Miaka 20 ya Mauaji ya Kimbari nchini Rwanda!


Serikali ya Rwanda imeanza Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 20 tangu yalipotokea mauaji ya kimbari nchini humo yaliyosababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao.

Maadhimisho haya yamezinduliwa na Rais Paul Kagame wa Rwanda aliyewasha mwenge utakaokimbizwa nchi nzima kama kielelezo cha Maadhimisho ya Mauaji ya Kimbari nchini Rwanda, kabla ya kuanza kipindi cha maombolezo ya kitaifa hapo tarehe 7 Aprili 2014.

Inakadiriwa kwamba, watu laki nane waliuwawa nchini Rwanda kati ya Mwezi Aprili na Juni 1994, wengi wao wakiwa wanatoka katika kabila la Watutsi. Televisheni ya taifa imeonesha baadhi ya matukio haya ambayo kwa takribani siku mia moja tu, maelfu ya watu walikuwa wamepoteza maisha na nchi kusambaratika kutokana na hofu za mashambulizi ya kikabila.

Miaka ishirini imepita, Rwanda imeanza kujielekeza katika mchakato wa ukweli na upatanisho, lakini wachunguzi wa mambo wanasema kwamba, kurasa chungu za mauaji ya kimbari bado hazifutwa katika mawazo ya wananchi wengi wa Rwanda. Wapinzani wa Serikali ya Rais Paul Kagame wanasema kwamba, bado anafanya hujuma kwa wapinzani wake, kwa kuwafutilia mbali na wala hakuna watu wanaowajibishwa kutokana na mauaji hayo!







All the contents on this site are copyrighted ©.