2014-01-07 08:56:23

Mshikamano na wananchi wa Sudan ya Kusini katika kipindi hiki kigumu!


Shirika la Kitume Kimataifa la Pax Christi linapenda kuonesha mshikamano wake wa dhati na wananchi wote wa Sudan ya Kusini wakati huu wanapokabiliana na machafuko ya kisiasa ambayo yamepelekea mauaji ya watu wasiokuwa na hatia na wengine wengi kulazimika kuyakimbia makazi yao. Inasikitisha kuona kwamba, kinzani za kisiasa zinageuzwa na kupachikwa masuala ya ukabila; mambo ambayo ni hatari sana kwa ustawi na maendeleo ya wengi.

Miaka miwili iliyopita, Sudan ya Kusini iliadhimisha uhuru wake, kwa kutaka kukazia misingi ya haki, amani, upatanisho na maendeleo ya wengi; demokrasia ikipewa msukumo wa pekee. Lakini mwishoni mwa Mwaka 2013, demokrasia na uhuru wa wananchi wa Sudan ya Kusini umegeuka kuwa ni maafa kwa watu wasiokuwa na hatia. Machafuko na kinzani za kisiasa na kijamii zimepelekea watu kuyakimbia makazi yao, hali ambayo inakwamisha jitihada za kujiletea maendeleo endelevu. Jumuiya ya Kimataifa inaonesha wasi wasi wake kutokana na kuzuka kwa vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Sudan ya Kusini.

Taarifa zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu elfu moja wamekwishapoteza maisha kutokana na vita inayoendelea Sudan ya Kusini. Mauaji ya watu kwa kisingizio chochote kile linasema Pax Christi ni ukiukwaji wa haki msingi za binadamu. Kumbe, kuna haja kwa pande zote zinazohusika na machafuko ya kisiasa nchini Sudan ya Kusini, kuketi kwa pamoja na kuanza mchakato wa majadiliano yatakayosaidia kusitisha umwagaji wa damu ya watu wasiokuwa na hatia.







All the contents on this site are copyrighted ©.