Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amewataka Watanzania
kuendelea kutoa maoni yao kuhusu aina ya Katiba wanayoitaka akisisitiza kuwa siyo
dhambi kwa watu kutoa maoni yanayopingana na mapendekezo ya Tume ya Mabadiliko ya
Katiba.
Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa tofauti na maneno yasiyokuwa ya kweli
ambayo yamekuwa yanasambazwa na baadhi ya watu kuwa kazi ya Katiba imekamilika, bado
Katiba mpya haijapatikana na wananchi wanaombwa kuendelea kutoa mapendekezo na maoni
yao.
Rais Kikwete ametoa ufafanuzi huo kuhusu mchakato wa kusaka Katiba mpya
nchini wakati alipokuwa anapokea Matembezi ya Vijana wa Chama cha Mapinduzi (CCM)
Kuadhimisha Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar katika sherehe iliyofanyika kwenye Viwanja
vya Maisala, mjini Zanzibar, Jumapili, Januari 5, 2014.
Akizungumza baada
ya risala za vijana ambazo zimesisitiza msimamo wa CCM kuhusu aina ya Muungano ambao
chama hicho kimeutetea tokea kuundwa kwake, Rais Kikwete amewaambia wananchi: “Tunataka
Katiba ya watu wote, siyo Katiba ya kikundi ama vikundi vya watu. Hivyo, toeni maoni
na mapendekezo yenu bila hofu wala woga kuhusu aina ya Katiba ambayo mnaitaka. Ni
haki yenu kutoa mawazo yenu bila hata kujali mtu mwingine anasema ama kufikiria nini.
Kila mtu ana uhuru wa kutoa maoni yake na hata kutofautiana na mapendekezo ya Tume
ya Mabadiliko ya Katiba siyo dhambi.”
Rais Kikwete amesema kuwa wananchi wanaweza
kutoa maoni yao kwa njia nyingi ikiwa ni pamoja na kupitia kwa wabunge wa Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar ambao
wote watakuwa ni wajumbe wa Bunge la Katiba.
Jumatatu iliyopita, Desemba 30,
2013, Tume ya Katiba iliyoongozwa na Makamu wa Kwanza wa Rais na Waziri Mstaafu, Mheshimiwa
Jaji Joseph Sinde Warioba ilimkabidhi Rais Kikwete Ripoti ya Tume hiyo ambayo ni pamoja
na Rasimu ya pili ya mapendekezo ya Katiba mpya.
Ameongeza Rais Kikwete: “Kuna
watu wameanza kupotosha wengine kwa kusema kuwa kazi ya Katiba imekamilika. La hasha.
Tume imetoa mapendekezo ambayo yanatakiwa kujadiliwa na kuamuliwa ipasavyo na Bunge
la Katiba. Bunge hilo lina mamlaka ya kuamua linavyoona inafaa kwa kifungu chochote
cha mapendekezo ya Tume.”
Amesisitiza Rais Kikwete: “Itumieni vizuri fursa
hii kutoa maoni yenu ili tupate Katiba inayotupatia Muungano imara na nchi ya kidemokrasia
na inayozingatia na kuheshimu haki za binadamu. Tupate Katiba ambayo itaendelea kuifanya
nchi yetu salama, tulivu na yenye kupata maendeleo shirikishi na kunufaisha wote.”
Katika
hotuba yake, Rais Kikwete pia amewakumbusha vijana historia ya vyama vya ukombozi
wa TANU na ASP, historia ya mahusiano kati ya vyama hivyo na watu wa Bara na Visiwani
na chimbuko la Muungano wa Tanzania ambao ulizaliwa Aprili 26, 1964 na mchango wa
Mapinduzi ya Zanzibar katika kuzaliwa kwa Muungano huo.
“Vile vile inatupasa
tukumbuke kuwa Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ndiyo yalikuwa chachu ya Muungano wa
nchi zetu mbili. Huwezi kuzungumzia Muungano bila Mapinduzi. Kama Mapinduzi yasingefanyika
Muungano usingekuwepo. Muungano ni mtoto wa Mapinduzi.”