Salini kwa ajili ya kuombea amani Sudan ya Kusini!
Waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutoka Sudan ya Kusini, wanaalikwa kwa namna
ya pekee kufunga na kusali kwa ajili ya kuombea amani na ustawi wa Sudan ya Kusini
hasa wakati huu ambapo nchi hii inakabiliwa na machafuko ya kisiasa ambayo yamepelekea
watu wengi kupoteza maisha na wengine wengi kuyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama
wa maisha!
Waamini wanaalikwa kusali hili kwamba, juhudi za kutafuta amani
kwa njia ya majadiliano zinazoendelea huko Ethiopia ziweze kuzaa matunda yanayokusudiwa,
yaani amani, ustawi na maendeleo ya wananchi wote wa Sudan ya Kusini.
Waamini
wanaombwa mahali popote walipo, wajikusanye na kusali kwa ajili ya nia ya kumlilia
Mwenyezi Mungu ili aweze kuwajalia wananchi wa Sudan ya Kusini amani ambayo waliitamani
kwa miaka mingi, lakini kwa sasa inaonekana kana kwamba inaweza kutoweka na matokeo
yake machafuko kutawala tena!