Maandalizi ya Jubilee ya Miaka 800 ya Wadominican yaanza kupamba moto!
Changamoto za utume wa Shirika la Wadominikani Barani Afrika ndiyo kauli mbiu itakayoongoza
Maadhimisho ya mkutano mkuu wa kumi na mbili wa Shirika hili utakaofanyika Jijini
Nairobi kuanzia tarehe 20 hadi 27 Julai 2014. Ni mkutano ambao utahudhuriwa na wawakilishi
wa Wadominikani Barani Afrika.
Hivi karibuni kamati ya Maandalizi imehitimisha
kikao chake kilichokuwa kinafanyika huko Johanesburg, Afrika ya Kusini. Huu pia utakuwa
ni mwanzo wa Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 800 tangu Shirika la Wadominikani lilipoanzishwa,
na kilele chake ni hapo Mwaka 2015.
Mtakatifu Domenico de Guzman, alianzisha
Shirika la Wadominikani lililotambuliwa kunako Mwaka 1215. Kunako Mwaka 1217 Papa
Onorio wa tatu, akaridhia Shirika la Wadominikani kuwa katika Orodha ya Mashirika
ya Kitawa ndani ya Kanisa, watawa ambao wanajikita katika kuhubiri Neno la Mungu.
Ufunguzi rasmi wa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 800 ya Wadominikan ni hapo tarehe
7 Novemba 2015 na kuhitimishwa tarehe 21 Januari 2017.