Mapambano dhidi ya umaskini wa hali na kipato nchini Marekani
Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Marekani, kwa Mwezi Januari 2014 linaendesha kampeni
dhidi ya umaskini nchini Marekani, kwa kujikita zaidi na zaidi katika kuhamasisha
mikakati ya maendeleo endelevu, itakayosaidia mchakato wa mapambo dhidi ya umaskini
wa hali na kipato nchini Marekani.
Juhudi hizi zinafanywa kwenye Parokia mbali
mbali nchini marekani, kwa kuhakikisha kwamba, kila Parokia inajitahidi kusoma alama
za nyakati kwa kuangalia hali ya umaskini wa watu wake, ili hatimaye, kuibua mbinu
mkakati utakaofanyiwa kazi na Kanisa Katoliki nchini Marekani. Takwimu zinaonesha
kwamba, kuna watu millioni 46.5 nchini Marekani wanaoishi katika hali ya umaskini.
Hawa ni sawa na asilimia 15% ya idadi ya wananchi wote wa Marekani.
Umaskini
huu ni mlolongo wa matatizo yanayowakabili wageni na wahamiaji; ukosefu wa fursa za
ajira mambo ambayo yanadhalilisha utu na heshima ya binadamu na kwamba, myumbo wa
uchumi kimataifa unaendelea kusababisha majanga mbali mbali nchini humo!
Baraza
la Maaskofu Katoliki Marekani linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema
kuonesha moyo wa upendo na mshikamano kwa wale wote wanaoteseka kutokana na umaskini
wa hali na kipato, ili wao pia waweze kuonja huruma na upendo wa Mungu kwa njia ya
ushuhuda unaotolewa na watu wenye mapenzi mema.
Wananchi wa Marekani hawana
budi kuunganisha nguvu zao ili kupambana na umaskini wa hali na kipato; kwa kusimama
kidete kulinda na kutetea zawadi ya maisha pamoja na haki msingi za binadamu. Maaskofu
wanakumbusha kwamba, tarehe 21 Januari 2014, Kanisa Katoliki nchini Marekani litafanya
kesha kwa ajili ya kuwaombea watoto ambao hawajazaliwa; watoto ambao wanapaswa kulindwa
na kutunzwa tangu pale wanapotungwa mimba tumboni mwa mama zao, hadi mauti ya kawaida
yanapowafika kadiri ya mpango wa Mungu.
Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani
linapenda kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Baba Mtakatifu Francisko kwa kutoa kipaumbele
cha kwanza kwa maskini katika mikakati, mipango na maisha ya Makanisa mahalia, ili
kuonesha upendo na mshikamano wa dhati. Maaskofu wanawahimiza waamini walei kuhakikisha
kwamba, wanashiriki kikamilifu katika maisha ya hadhara, ili waweze kuchangia katika
ustawi na maendeleo yao: kiroho na kimwili, lakini zaidi katika mapambano dhidi ya
umaskini wa hali na kipato!