Watanzania wanaomboleza kifo cha waziri wa fedha, Dr. William Mgimwa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amepokea kwa mshtuko
na huzuni kubwa taarifa za kifo cha Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dr. William Mgimwa,
aliyekuwa pia Mbunge wa Jimbo la Kalenga (Mkoa wa Iringa) kupitia Chama cha Mapinduzi
(CCM).
Rais Kikwete amesema kuwa taifa limempoteza Waziri Mgimwa katika kipindi
lilipokuwa linamhitaji zaidi kutokana na mchango wake mkubwa ambao amekuwa akiutoa
kupitia nafasi zake za Waziri wa Serikali na mwakilishi wa wananchi wa Jimbo la Kalenga.
Kifo
cha Mheshimiwa Mgimwa kimetangazwa Jumatano, Januari Mosi, 2014, na Katibu Mkuu Kiongozi
(KMK) Balozi Ombeni Sefue kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katika tangazo lake, Balozi Sefue amesema kuwa Waziri Mgimwa ameaga dunia asubuhi
saa 5:20 (Saa za Afrika ya Kati) katika Hospitali ya Kloof Medi-Clinic , Pretoria,
Afrika Kusini ambako amekuwa amelazwa kwa muda sasa.
Balozi Sefue amesema kuwa
maandalizi ya kuurudisha nyumbani mwili wa Waziri Mgimwa yanafanywa na Serikali kwa
kushirikiana na familia yake na kuwa taarifa zaidi kuhusu suala hilo zitatolewa baadaye
kwa kadri zinavyopatikana na maandalizi yanavyoendelea.
Katika salamu zake
kwa Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda na kwa familia ya Marehemu Mgimwa, Rais
Kikwete amesema: “Sina maneno ya kutosha kuelezea mshtuko na huzuni yangu kubwa kufuatia
taarifa za kifo cha Mheshimiwa Mgimwa. Binafsi nimemtembelea mara mbili kwenye Hospitali
alikokuwa amelazwa na mara ya mwisho hali yake ilikuwa imeimarika. Tulizungumza kwa
kiasi cha dakika 10 hivi akanielezea nia yake na tamaa yake ya kurejea nyumbani kwa
sababu hali yake ilikuwa nzuri.”
Ameongeza Mheshimiwa Rais Kikwete: “Sote tunajua
mchango wake katika Serikali. Sote tulitamani kuendelea kuwa naye, lakini haya ni
mapenzi ya Mungu.” “Napenda kutoa pole nyingi na rambirambi zangu za dhati kwa wana-familia
wote kwa kuondokewa na mhimili wao. Naungana nanyi katika kuomboleza msiba huo mkubwa.
Napenda mjue kuwa msiba huu ni msiba wangu pia. Machungu yenu ni majonzi yangu,” amesema
Rais Kikwete. Rais pia amewatumia rambirambi wananchi wa Jimbo la Kalenga akisema
kuwa wamempoteza mwakilishi na mtetezi mahiri wa maslahi yao. Historia fupi ya
Waziri wa Fedha wa Tanzania, Dr. William Mgimwa aliyefariki dunia nchini Afrika Kusini
alipokuwa amelazwa kwa matibabu:
Kuzaliwa: Januari 20, 1950 Kalenga, Mkoani
Iringa. Elimu: 1966 - 1967 Shule ya Msingi Tosa 1961 -1965 Shule ya Msingi
Wasa 1970-1971 Seminari ya Mafinga 1968 - 1969 Tosamaganga Sekondari 1975
- 1984 Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) - Postgraduate in Finance 1989 - 1991
IDM Mzumbe (MBA - Finance) Ajira 1981 - 2000 - NBC Ltd (Mhasibu, Mhadhiri, Mkurugenzi,
Mkurugenzi Mkuu) 2000 - 2010 - Chuo cha Benki Kuu ya Tanzania Mwanza (Mkuu wa Chuo) 2010
- 2013 - Mbunge, Kalenga (CCM) Kufariki: Januari 1, 2014(P.T)