2014-01-02 10:32:53

Siku kuu ya Jina takatifu la Yesu, Wayesuit kumwimbia Mungu utenzi wa shukrani kwa ajili ya neema za Mtakatifu Pietro Favre!


Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Jina Takatifu la Yesu, hapo tarehe 3 Januari 2014 anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa la Yesu lililoko mjini Roma majira ya asubuhi, kama shukrani kwa neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kutangazwa kwa Mwenyeheri Pietro Favre kuwa Mtakatifu. RealAudioMP3
Padre Adolfo Nicolàs katika barua yake ya shukrani kwa Mama Kanisa kumtangaza Mwenyeheri Pietro Favre kuwa Mtakatifu; uamuzi uliofanywa na Papa Francisko kwa kufuata sheria mlingano anasema, Mtakatifu Favre awe ni changamoto na mfano wa kuigwa kwa Wayesuiti mmoja mmoja na katika ujumla wao, katika hija ya mabadiliko ya maisha ya kiroho.
Hili ni tukio ambalo linafuatia tukio jingine kubwa la kihistoria la mabadiliko makubwa yaliyofanyika kunako mwaka 1814, changamoto ya kuendelea kujikita katika maisha ya imani kwa Mwenyezi Mungu, daima wakijitahidi kuwa ni wakweli na watu wazi; kwa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani!
Ni Mtakatifu ambaye ameacha urithi wa kudumu katika Shirika la Wayesuit. Mtakatifu Favre ni kati ya wafuasi wa Mtakatifu Inyasi kama vile alivyokuwa Mtakatifu Francisko Xsaveri. Kwa miaka mitano wakawa pamoja kwenye Chuo Kikuu cha Paris, Ufaransa na kushiriki Fumbo la Ekaristi Takatifu, hapo tarehe 15 Agosti 1534.
Wakati Mtakatifu Inyasi alipokuwa anakwenda nyumbani kwao Azpeitia, Mwezi Machi 1535, akaacha Shirika mikononi mwa Jaalim Pietro Favre, ili kuliendeleza: kiroho na kimwili. Akaonesha moyo wa udugu na urafiki, tayari kuanza mchakato wa ujenzi wa Jumuiya ya Wayesuit, kama mahali pa kukutana na kuzungumza na Mwenyezi Mungu. Mtakatifu Favre alikuwa ni mtu wa sala, aliyetajirisha maisha yake kwa njia ya sala na Ibada kwa Bikira Maria, bila kuwasahau watakatifu na wafiadini.
Ni mtu aliyesali kwa ajili ya Kanisa, Viongozi na Shirika lake. Akawakumbuka waliotopea katika ukanimungu bila kuwasahau waliokuwa wananyanyaswa na kuteswa kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Ni Mtakatifu aliyeamini katika maisha ya sala kama njia muafaka ya kukutana na kuzungumza na Mwenyezi Mungu. Yesu Kristo akawa ni msingi na nguzo ya maisha na utume wake ndani ya Kanisa. Hali ambayo ilijionesha kwa namna ya pekee katika: Katekesi, Maandiko Matakatifu,Mahubiri. Mafundisho na Huduma kwa Jirani.
Padre Adolfo Nicolàs anasema, Mtakatifu Pietro Favre ataendelea kukumbukwa kama Kaka yao mkubwa na kwamba, uwepo wake endelevu ndani ya Shirika ni baraka na neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Ni kielelezo cha utii na unyenyekevu kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.








All the contents on this site are copyrighted ©.