Jimbo kuu Katoliki Arusha, baada ya Jubilee ya Miaka 50, linajipanga kuadhimisha Sinodi
ya pili ya Jimbo!
Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu Katoliki Arusha katika mahojiano maalum na
Radio Vatican anabainisha kwamba, baada ya kilele cha Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka
50 ya uwepo na utendaji wa Jimbo kuu Katoliki Arusha, sasa wanajipanga kusheherekea
Sinodi ya Pili ya Jimbo kuu la Arusha, ili kupanga mikakati ya kichungaji na maendeleo
kwa Familia ya Mungu, Jimbo kuu Katoliki Arusha.
Jubilee ya
miaka 2000 ya Ukristo ilikuwa ni chachu ya mikakati ya kichungaji iliyopelekea Maadhimisho
ya Sinodi ya kwanza ya Jimbo kuu Katoliki Arusha. Baada ya kilele cha Maadhimisho
ya Jubilee ya Miaka 50 ya uwepo na utendaji wa Jimbo kuu Katoliki Arusha, sasa Familia
ya Mungu inajipanga kupembua mafanikio, mapungufu na changamoto zilizojitokeza katika
kipindi cha Miaka 50 iliyopita, tayari kutweka hadi kilindini kwa kujiwekea mpango
mkakati wa shughuli za kichungaji na maendeleo kwa Miaka 10 ijayo!
Askofu mkuu
Lebulu anasema, dhana ya Familia ya Mungu itaendelea kupewa kipaumbele cha kwanza,
kwani hapa kila Mwana familia anahamasishwa kushiriki kikamilifu katika ustawi na
maendeleo ya Jimbo kuu Katoliki la Arusha, ili kujenga na kuimarisha sura ya Kanisa
la Kristo. Roho Mtakatifu ataendelea kusaidia juhudi na mikakati hii kwani Familia
ya Mungu Jimbo kuu Katoliki Arusha inatambua kwamba, wao ni sawa na vyombo vya udongo
lakini wanahifadhi hazina kubwa ambayo ni Kristo mwenyewe, anayepaswa kupendwa, kuheshimiwa,
kutukuzwa na kutangazwa kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili!
Kilele cha Maadhimisho
ya Jubilee ya Miaka 50 ya uwepo na utendaji wa Jimbo kuu Katoliki Arusha, kilikuwa
ni hapo tarehe 29 Desemba, 2013 wakati Kanisa lilipokuwa linaadhimisha Sherehe ya
Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. Ibada iliongozwa na Kardinali Polycarp
Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam na mahubiri kutolewa na Askofu mkuu
Yuda Thaddeus Ruwaichi wa Jimbo kuu la Mwanza. Ibada hii imehudhuriwa na Maaskofu
17 na Mapadri zaidi ya 80 pamoja na umati mkubwa wa watawa na waamini walei!
Katika
salam zake, Askofu mkuu Francisco Padilla, Balozi wa Vatican nchini Tanzania, alikazia
kwa namna ya pekee udugu kama msingi na njia ya amani unaopaswa kupata chimbuko lake
kutoka ndani ya Kanisa. Anasema, siasa na mikakati ya kiuchumi visiishie kwenye teknolojia
na kutelekeza tunu na hatima ya kazi ya binadamu; mambo ambayo yanaweza kusababisha
chuki na husuda miongoni mwa wananchi bali sera na mikakati ya kiuchumi iwe ni kikolezo
cha upendo na mshikamano wa kidugu kati ya wananchi wa Tanzania.
Askofu mkuu
Padilla amekazia pia umoja, udugu na mshikamano wa kitaifa, ili kujenga na kuimarisha
misingi ya haki, amani na upatanisho. Watanzania waendelee kushikamana kama ndugu,
kwa kuheshimu na kuthamini mawazo ya jirani zao; kwa kusaidiana na kusameheana ili
kudumisha udugu na amani ambavyo watanzania wamekuwa wakijivunia kwa miaka mingi!
Naye
Askofu Oral Sosy wa Kanisa la TAG, Arusha ambaye ni Katibu wa Umoja wa Madhehebu ya
Kikristo Mkoani Arusha katika salam zake kwa Jimbo kuu la Arusha anasema, Umoja wao
una kazi kuu tau: kuhubiri amani, kuombea Serikali na Nchi ya Tanzania kwa ujumla
sanjari na kuangalia masuala ya kijamii.
Umoja huu unaendelea kufuatilia kwa
umakini mkubwa mchakato wa Katiba Mpya ya Tanzania. Mambo ambayo wasingependa kuona
yanawagawa na kuachanganya watanzania ni: ndoa za watu wajinsia moja, utamaduni wa
kifo na masuala ya dini au madhehebu kuingizwa kwenye Katiba ambayo kimsingi ni Sheria
Mama.
Kwa upande wake, Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amepongeza Umoja
wa Madhehebu ya Kikristo mkoani Arusha kwa kujikita katika: udugu, amani na mshikamano
miongoni mwa waamini. Waziri mkuu ambaye alikuwa anamwakilisha rais Jakaya Kikwete
wa Tanzania amelipongeza Jimbo kuu Katoliki la Arusha kwa kuasisi Umoja wa Wakristo,
mfano wa kuigwa na Mikoa mingine nchini Tanzania. Viongozi wa kidini wasaidie kujenga
uchaji wa Mungu miongoni mwa waamini wao, kwani huu ni msaada mkubwa kwa Serikali
katika kulinda na kudumisha misingi ya haki na amani.