2013-12-30 10:10:02

Maandalizi ya Siku ya Familia Kimataifa kwa Mwaka 2015 yanaendelea kupamba moto!


Familia ya Mungu Jimbo kuu la Philadelphia nchini Marekani inaendelea na maandalizi kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani, itakayoadhimishwa nchini Marekani, mwezi Septemba 2015. RealAudioMP3
Hili ni tukio ambalo Kanisa mahalia linashirikiana kwa karibu zaidi na Baraza la Kipapa la familia ili kuhakikisha kwamba, mambo yanakwenda sawia. Jimbo kuu la Philadelphia limewateuwa Bibi Donna Farrel na Bwana Jack O’Brien kuwa wakurugenzi waku katika Maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani kwa Mwaka 2015.
Askofu mkuu Charles Chaput wa Jimbo kuu la Philadelphia anasema, kwa sasa wanasubiri kupata ratiba kamili ya Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho haya na kwamba, hili linatarajiwa kuwa ni tukio la aina yake kwa maisha na utume wa Jimbo kuu la Philadelphia na Marekani katika ujumla wake. Hii inatokana na ukweli kwamba, Baba Mtakatifu Francisko anapenda kujihusisha na watu wa kawaida pasi na makuu.
Maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani ni Jukwaa muafaka ambalo litamwezesha Baba Mtakatifu kujisikia kweli yuko nyumbani, ili kushirikiana nao katika kutangaza Injili ya Furaha pamoja na kuendelea kupambana na kinzani na vizingiti vya tunu msingi za maisha ya kifamilia kwa ujasiri mkuu pasi na kukata wala kukatishwa tamaa. Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, ndoa na familia ni taasisi zinazokabiliana na changamoto nyingi mintarafu mambo ya maadili na utu wema; sheria na changamoto za kiuchumi na kijamii.
Maana ya ndoa inaanza kuwa ni tungo tata kwa maana kwamba, maana yake ya asili inaanza kumeng’enyuliwa na kuondolewa katika mpango wa Mungu katika kumshirikisha mwanadamu kwenye kazi ya Uumbaji. Ndoa sasa inakuwa ni mahali pa kutaka ”kujifurahisha na kujirusha” pasi na maadili wala dhamana!
Askofu mkuu Chaput anasema, Baba Mtakatifu Francisko kwa kutambua umuhimu, fursa, changamoto na vikwazo vinavyowakabili wanandoa, ameamua kuitisha Sinodi maalum kwa ajili ya Familia, itakayofanyika mjini Vatican mwezi Oktoba, 2014. Utakuwa ni muda muafaka kwa Kanisa kutafakari tena juu ya Mafundisho ya Ndoa na Familia na jinsi ya kuyamwilisha katika uhalisia wa maisha na utume wa Kanisa.
Ni nafasi ya kupembua kwa kina ni mafundisho yepi ambayo yanakabiliana na kinzani kutoka katika Jamii na sababu zake. Mababa wa Sinodi watatakiwa kuibua mbinu mkakati wa kuhakikisha kwamba, Mafundisho haya yanaeleweka vyema zaidi. Maadhimisho haya ni awamu ya kwanza itakayoweka msingi wa Maadhimisho ya Awamu ya Pili yatakayofanyika kunako Mwaka 2015. Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa Kitume Injili ya Furaha anakazia umuhimu wa umoja na mshikamano wa Maaskofu katika maisha na utume wa Kanisa, pengine huu utakuwa ni mwanzo wa utekelezaji wa dira na mwelekeo huu mpya, changamoto kutoka kwa Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na ushauri uliotolewa na Makardinali wakati wa mikutano elekezi kabla ya uchaguzi wa Baba Mtakatifu Francisko.
Baraza la Kipapa la Familia limekwisha watumia Maaskofu mahalia hati ya mwongozo wa Sinodi inayofanyiwa kazi kwa sasa ili hatimaye, Sekretarieti ya Maaskofu iweze kuyachambua na kutoa hati ya kutendea kazi, yaani ”Instrumentum Laboris”. Ni mwongozo unaogusia: maana, asili ya ndoa na familia; changamoto zilizoko. Maaskofu wanaalikwa kujibu maswali dodoso kwa kuwashirikisha waamini wao. Majibu haya yatasaidia kukoleza majadiliano wakati wa Sinodi maalum ya Familia itakayofanyika Oktoba 2014.
Mchakato huu wa kukusanya maoni si kura ya maoni kwa ajili ya kutengua Mafundisho Tanzu ya Kanisa, bali ni nyenzo muhimu inayotaka kulisaidia Kanisa kuona fursa, vikwazo na changamoto katika maisha ya ndoa na familia. Ni maswali ambayo yamerahisishwa ili kuwawezesha waamini kuyajibu kwa ufasaha bila kupotosha maana iliyokusudiwa na Baraza la Kipapa la Familia.
Askofu mkuu Charles Chaput anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuendelea kumkumbuka Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na sala zao hasa wakati huu anapojadili masuala tete katika maisha na utume wa Kanisa.








All the contents on this site are copyrighted ©.