Yaliyojiri Jimboni Dodoma, Siku kuu ya Utoto Mtakatifu!
Watoto 1,500 kutoka Parokia mbali mbali za Jimbo Katoliki Dodoma, Ijumaa tarehe 27
Desemba 2013 wameshiriki katika Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kufanya kumbu
kumbu ya Watoto mashahidi waliouwawa kikatili na Mfalme Herode, kutokana na wasi wasi
wa kudhani kwamba, Mtoto Yesu alikuwa anakuja kumpora madaraka yake!
Ibada
ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Parokia ya Mtakatifu Gaspar del Buffalo, Makole,
imeongozwa na Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma. Watoto wametakiwa
kuonesha moyo wa shukrani kwa wazazi na walezi wao, bila kusahau kuwa na ibada pamoja
na uchaji kwa Mwenyezi Mungu anayewakirimia neema na baraka katika hija ya maisha
yao hapa duniani. Mungu ni Baba mwenyezi anayawaongoza watoto wake katika njia ya
amani, haki na utakatifu.
Askofu Nyaisonga katika mahubiri yake, amewataka
watoto kuonesha moyo wa shukrani kwa wazazi na walezi wao kutokana na: tunza na malezi
bora wanayowakirimia; ikiwa ni pamoja na elimu, afya pamoja na mahitaji yao msingi,
bila kusahau kwamba, imani waliyonayo ni urithi mkubwa kutoka kwa wazazi wao, changamoto
ya kuilinda, kuikuza na kuendeleza.
Mtoto Yesu alipozaliwa, amri ilitoka kwa
Mfalme Herode aliyekuwa amesikia habari kutoka kwa Mamajusi kuhusu kuzaliwa kwa Mfalme
wa Wayahudi, jambo ambalo lilimhuzunisha sana, kiasi cha kuingiwa na hofu pamoja na
wasi wasi mkubwa. Matokeo yake akaamuru watoto wote waliokuwa na umri chini ya miaka
miwili wauwawe. Lakini kwa maongozi na tunza ya Mwenyezi Mungu, Mtoto Yesu aliweza
kuokolewa na Mtakatifu Yosefu na Bikira Maria waliokimbilia ugenini nchini Misri.
Askofu
Nyaisonga anasema, hata baada ya miaka zaidi ya elfu mbili kupita, bado kuna akina
Herode wanaoendelea kujitokeza duniani kwa kukumbatia utamaduni wa kifo unaosimikwa
katika sera za utoaji mimba, ubinafsi, uchoyo na mmong'nyoko wa maadili na utu wema.
Kuna maelfu ya watoto wanaopoteza maisha yao sehemu mbali mbali za dunia kwa kutolewa
mimba; kuna kundi kubwa la watoto linaloishi katika mazingira hatarishi na kwamba,
kuna watoto ambao wamekata tamaa na matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi. Watoto
wote hawa wamekumbukwa katika sala na sadaka iliyotolewa kwa ajili yao!
Askofu
Nyaisonga amewataka watoto waliobahatika kupata urithi wa imani na matunzo bora ya
kifamilia, kusimama kidete kulinda na kutetea imani yao na kamwe wasikubali kuyumbishwa
na watu wanaofanana na akina Herode, waliomezwa na ubinafsi kiasi cha kutaka kukatisha
maisha ya watoto kinyume cha mpango na mapenzi ya Mungu. Wazazi na walezi wajenge
tabia ya kuwapenda, kuwaheshimu na kuwathamini watoto! Wawasaidie kukuza karama na
vipaji vyao; wawe mstari wa mbele kuwapatia mahitaji yao msingi pamoja na kuhakikisha
kwamba, haki msingi za watoto zinalindwa na kuheshimiwa.
Katika Ibada hii ya
Misa Takatifu, Watoto 119 waliimarishwa katika Ukristo wao kwa kupewa Sakramenti ya
Kipaimara inayokuza na kuzamisha zaidi neema ya Sakramenti ya Ubatizo: kwa kufanyika
waana wa Mungu na ndugu zake Kristo; kwa kupokea mapaji ya Roho Mtakatifu na kuunganishwa
zaidi na Kanisa. Sakramenti ya Kipaimara inawapatia waamini nguvu ya pekee kutoka
kwa Roho Mtakatifu kwa ajili ya kueneza na kutetea Imani kwa maneno na matendo kama
Mashahidi wa kweli wa Kristo bila kuuonea aibu Msalaba wa Kristo. Wakristo hao wamepokea
mhuri wa Roho Mtakatifu.
Katika Ibada hii ya Misa Takatifu, Wanachama wapya
wa Shirika la Kipapa la Utoto Mtakatifu Jimbo Katoliki Dodoma walipokelewa rasmi na
wale wa zamani wamerudia ahadi zao. Makamu Mwenyekiti Baraza la Walei, Jimbo Katoliki
Dodoma alikula kiapo cha utii. Maskauti wapya walipata pia fursa ya kula kiapo pamoja
na kupandishwa vyeo. Chama cha Skauti ni matunda ya kazi na utume wa Askofu Nyaisonga,
Jimbo Katoliki Dodoma, kwa lengo la kutaka kuwashirikisha watoto katika maisha na
utume wa Kanisa.
Jimbo Katoliki Dodoma limezindua pia Programme ya Neno la
Mungu kwa njia ya kusikiliza, ili kutoa fursa kwa waamini, vikundi na watu wenye mapenzi
mema kusikiliza Neno la Mungu kwa njia ya kisasa. Hii ni Programe iliyoandaliwa na
Chama cha Biblia Mkoa wa Dodoma, chini ya Mwenyekiti wake mpya Askofu Bernardine Mfumbusa
wa Jimbo Katoliki Kondoa.