2013-12-28 09:41:48

Hija ya kiroho katika mazingira ya Yesu kwenye Nchi Takatifu


Mahujaji 55 kutoka Tanzania wanaotembelea Nchi Takatifu kama sehemu ya mchakato wa kukuza na kuimarisha imani, tayari kuitolea ushuhuda katika maisha wanasema, hija hii ya maisha ya kiroho imekuwa na mafanikio makubwa katika maisha yao. Wamepata nafasi ya kusali mahali alipozaliwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia pamoja na kutembelea maeneo matakatifu Mjini Yerusalem.

Mahujaji hao wamekwenda hadi Bethania, nyumbani kwao Martha na Maria; wakaona kaburi la Lazaro. Wanasema, hapa wamekumbushwa umuhimu wa sala na kazi, kama ambavyo Yesu mwenyewe alifafanua alipokuwa anazungumza na Maria aliyekuwa amechagua fungu bora zaidi sanjari na kujenga urafiki wa dhati na Yesu, hali ambayo ilimfanya hata Yesu kumlilia rafiki yake Lazaro. Watu waguswe na majanga ya jirani zao na hivyo kuepukana na utandawazi usiojali wala kuguswa na shida za wengine kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko.

Mahujaji hao wa Tanzania wamepata fursa ya kutembelea mjini Yeriko; wakapanda Mlimani ambako Yesu baada ya kufunga kwa siku arobaini mchana na usiku bila kula, alishawishiwa na Ibilisi, lakini akashinda mitego yote ya Ibilisi. Waamini wanakumbushwa umuhimu wa kusali na kufunga kama njia ya kudhibiti vilema na mapungufu yao ya kibinadamu.

Mahujaji wametembelea Bahari ya Sham, wakakumbushwa umuhimu wa Sakramenti ya Ubatizo na jinsi Waisraeli walivyookolewa kutoka utumwani Misri kwa mkono wa nguvu na maajabu kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo wanatumwa kuwa ni Manabii, Wafalme na Makuhani katika Familia, Jumuiya na Mahali pao pa kazi, tayari kumshuhudia Kristo na Kanisa lake kwa njia ya maisha adili.

Mahujaji hawa katika mahojiano maalum na Radio Vatican wanasema wamevutiwa sana na mapango ya Jumuiya ya Qumran, mahali ambapo wataalam waligundua Maandiko Matakatifu yaliyokuwa yamehifadhiwa kwenye Mapango. Wamekumbushwa umuhimu wa kusoma, kutafakari na kumwilisha utajiri wa Neno la Mungu katika maisha yao ya kila siku! Wanasema, eneo hili ni Jangwa sana, kiasi cha kushindwa kutambua ile ahadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kuhusu "asali na maziwa".

Kwa hakika, hija hii ya maisha ya kiroho, imekuwa ni kikolezo kikubwa cha imani katika matendo; kwa sasa wana upeo na ufahamu mkubwa kuhusu mazingira ya Yesu na Maandiko Mtakatifu kwa ujumla wake! Waisraeli ni watu wanaoishi katika mazingira magumu, lakini Mwenyezi Mungu amewajalia kipaji cha akili na ugunduzi, kiasi kwamba, daima wanajitahidi kuendeleza ile kazi ya uumbaji, laiti kama amani, utulivu vingekuwepo, bila shaka Waisraeli leo hii wangekuwa mbali katika maendeleo! Ni mshangao wa baadhi ya mahujaji kutoka Tanzania huko Nchi Takatifu!

Mahujaji 55 kutoka Tanzania wanajiandaa kwenda Galilaya, huko ambako Yesu alitumia muda wake mwingi kuhubiri; hapa wanatarajia kula samaki na wanandoa watano wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, watarudia tena ahadi zao za Ndoa, tayari kumshuhudia Kristo na Kanisa lake kwa maisha ya kifamilia kadiri ya mpango wa Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.