2013-12-27 09:58:10

Jubilee ya Miaka 50 Jimbo kuu la Arusha: Changamoto ni hofu na vizingiti vya mila na tamaduni... Lakini! Angalia na ushangae mwenyewe!


Waswahili wana mambo! Eti penye msafara wa Mamba, hapo hapo Kenge hakosi! Leo katika mahojiano maalum kati ya Radio Vatican na Askofu mkuu Josephat Louis Lebulu wa Jimbo kuu Katoliki Arusha, Tanzania wakati huu wanapojiandaa kwa kilele cha Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Uwepo na Utendaji wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha, anazungumzia changamoto kuu mbili: hofu na utamadunisho! RealAudioMP3

Askofu mkuu Lebulu anasema kwamba, pale ambapo Yesu anachapa kazi yake barabara, hapo kwa hakika Shetani hawezi kukosekana ili kuvuruga kazi njema inayofanywa na Yesu kwa njia ya wafuasi wake. Mlipuko wa bomu uliotokea wakati wa kutabaruku Kanisa la Parokia ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi, ulikuwa ni mkono wa Iblisi, kutaka kuwaogopesha waamini wasifurahie na kuzama katika furaha ya ukombozi. Hizi zilikuwa ni jitihada za makusudi za kufisha ari na mwamko wa imani Jimbo kuu Katoliki la Arusha.

Askofu mkuu Lebulu anasema, Kanisa lililolipuliwa kwa bomu, kilikuwa ni kielelezo wazi cha Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya uwepo na utendaji wa Jimbo kuu Katoliki Arusha. Waamini walikuwa wamekusanyika kumshukuru Mungu kwa zawadi ya Imani Katoliki, hapo wakalipuliwa kwa bomu, ili kuwajengea hofu na mashaka makubwa.

Badala ya waamini kukata na kukatishwa tamaa na vitendo hivi, badala yake, waamini wameshinda hofu na wasi wasi; wamepata ari na mwamko mpya, tayari kujitosa kimasomaso kushuhudia imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, bila woga wala makunyanzi kwani wanasema, ikiwa kama Kristo akiwa upande wao! Mwanadamu atawatenda nini? Badala ya kukatishwa tamaa, waamini wameimarishwa zaidi katika imani!

Askofu mkuu Lebulu anaendelea kusema kwamba, kuna baadhi ya waamini wanakata tamaa kwa kudhani kwamba, hatua waliyofikia katika imani bado ni kidogo sana na kwamba, imani kwa kiasi kikubwa bado inayumba na kukutana na vizingiti katika mila na tamaduni nyingi za waamini wa Jimbo kuu Katoliki la Arusha. Kuna mambo mengi bado yanasigana na kweli za Kiinjili na kumbe, hii ni changamoto kutoka katika undani wa maisha ya waamini wenyewe na hii ni kali zaidi kuliko hofu ya kifo!

Askofu Mkuu Lebulu anasema, inachukua muda mrefu kubadili mila, tamaduni na desturi za watu. Jimbo kuu Katoliki Arusha, linamwomba Yesu mwenyewe aguse tamaduni zao, ili kuwakomboa, kwani amekuja kuwakomboa watu na mazingira yao. Bado kuna changamoto ya kuendelea kutamadunisha Injili, ili kusafisha na kukatasa yale mambo ambayo yanasigana na tunu msingi za Kiinjili.







All the contents on this site are copyrighted ©.