2013-12-26 10:39:29

Mkutano wa Vijana wa Taizè waanza kutimua vumbi!


Kuanzia tarehe 28 Desemba hadi tarehe Mosi, Januari 2014, Vijana kutoka Bara la Ulaya watakuwa wanafanya mkutano wa 36 wa Vijana ulioandaliwa na Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè huko Strasburg, Ufaransa. Vijana watakapofika mjini humo watapokelewa na kupewa hifadhi na familia pamoja na taasisi mbali mbali na baadaye kushiriki katika sala ya jioni. RealAudioMP3

Wakati wote huu, vijana watakuwa wanashiriki katika Ibada za Misa Takatifu kwenye Parokia mbali mbali na jioni watakuwa wanakusanyika kujadili kuhusu tasahufi ya maisha ya kiroho: Watagusia pia masuala ya kijamii, kihistoria na kisanaa Barani Ulaya.

Vijana watakuwa na fursa ya kusali kwa pamoja kwenye Uwanja wa Wacken. Jumatatu tarehe 30 Desemba na Jumanne tarehe 31 Desemba, 2013, Vijana watakuwa na ratiba maalum ya kusali kwa ajili yakuombea amani duniani pamoja na kuadhimisha Siku kuu ya Wenyeji itakayoenea sehemu mbali mbali ambazo vijana watakuwa wanaonjeshwa ukarimu na wananchi wa Ufaransa katika ujumla wao.

Tarehe Mosi, Januari 2014 baada ya kupata chakula cha mchana kwenye familia na taasisi zinazowakirimia, vijana watakunja virago na kuanza safari ya kurudi kwenye nchi zao, tayari kumwilisha uzoefu na mang’amuzi ya maisha ya kiroho waliyofainikiwa kupata katika kipindi hiki.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Vijana wa Jumuiya ya Taizè anawakumbusha juu ya Maadhimisho ya Siku ya 35 ya Vijana wa Taizè yaliyofanyika mjini Roma kwa kusali pamoja na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Papa Francisko anasema, kwa hakika Roma wakati ule ilisheheni umati wa vijana kutoka sehemu mbali mbali za Bara la Ulaya.

Baba Mtakatifu anawaambia vijana hawa kwamba, anawategemea katika ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake; ili kujenga na kuimarisha moyo wa amani na upatanisho, ili hatimaye, Injili iweze kuota mizizi yake kwenye mioyo ya vijana wengi Barani Ulaya.

Mheshimiwa Martin Junge, Katibu mkuu wa Shirikisho la Makanisa ya Kiluteri Duniani anawapongeza vijana kwa kuamua kushiriki katika tukio hili la kidini linalobubujika furaha ya pekee kwani: vijana wanapotembea huku wakisali na kuimba, watakuwa wanashiriki katika mchakato wa kujenga na kudumisha mshikamano mpya. Mheshimiwa Junge anawatakia kila la kheri na baraka tele katika ujenzi wa dunia mpya inayosimikwa katika haki, amani na mshikamano wa dhati.

Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa katika salam zake anabainisha kwamba, teknolojia ya mawasiliano imekuwa na kupanuka kiasi cha kuwafanya watu kujisikia kuwa wa moja. Changamoto iliyoko mbele ya Jumuiya ya Kimataifa ni kujenga na kuimarisha moyo wa huruma na uraia wa kimataifa. Lengo liwe ni kuunganisha dunia, huku watu wenyewe wakiwa wameungana. Watu wana malengo tofauti ya maisha, lakini hawana budi kujenga na kuimarisha ushirikiano mpana zaidi, hii ndiyo mantiki ya utandawazi kwa sasa.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema kwamba, anawategemea vijana kumwilisha malengo msingi ya Umoja wa Mataifa katika kukuza na kudumisha misingi ya amani, maendeleo endelevu na haki msingi za binadamu.

Bwana Herman van Rompuy, Rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya katika ujumbe wake kwa vijana wa Taizè wanakutanika mjini Strasburg, Ufaransa anawataka vijana kuvuka kizingiti cha utengano; kwa kukazia upatanisho na umoja miongoni mwa Wakristo ili kujenga Kanisa moja, kadiri ya kauli mbiu inayoongoza Maadhimisho ya 36 ya Vijana wa Taizè Barani Ulaya.

Kauli mbiu inakazia pamoja na mambo mengine umoja katika utofauti; na umoja kwa njia ya neema katika utofauti. Haya ni mambo ambayo Baraza la Ulaya limeendelea kuyafanyia kazi kama sehemu ya vipaumbele vyake katika ujenzi na maendeleo ya Ulaya.








All the contents on this site are copyrighted ©.