2013-12-24 08:22:00

"THE BREAKING NEWS"


MERRY CHRISTMAS – HERI KWA NOELI! Kristmas ni Birthday ya mmoja katika UTATU aliyetumwa kufanya kazi kwenye sayari hii inayoitwa dunia. Hebu tujaribu kupiga twasira. Siku moja, huko mbinguni kulikuwa na mkutano wa Halmashauri kuu ya Utatu Mtakatifu. RealAudioMP3

Ajenda kuu ya mkutano ilihusu kuizungumzia sayari dunia. Hasa kutokana na mabadiliko makuu yaliyokuwa yanajitokeza hapa na pale baada ya uumbaji. Ikabidi Utatu uangalie hatima yake na kutolea maamuzi. Uamuzi ambao ulitegemewa ubadili mfumo mzima wa maisha ya binadamu duniani! Kwa vile ulikuwa mkutano wa kwanza toka kazi ya uumbaji ilipokamilika, ilibidi kwanza kutathmini mwendo mzima wa uumbaji ulivyokuwa.

Mwishoni ikathibika kwamba ni kweli “Mbingu na nchi zilishaumbwa. Awali nchi hiyo ilikuwa ukiwa, tena utupu, na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji.” Na utatu ukakiri kwamba ulitamka kwa pamoja, “Iwe Nuru!” (Mwa 1:30). Baada ya kuiumba Nuru “Utatu ukaiona nuru, ya kuwa ni njema;” (Mwa 1:4). Halmashauri ikajipongeza kwa kazi hiyo nzuri na kwamba sasa Nuru ilikuwa imeshaifukuza giza huko duniani.

“Hiyo ilikuwa Nuru halisi, amtiaye nuru kila mtu hapa ulimwengu” (Yoh. 1:9). Nuru hiyo ni alama ya uhai, ukweli, uwazi, haki, upendo, matumaini, furaha, uzuri, maisha bora kwa kila mkaaji wa duniani. Lakini katika tathmini hiyo ikagundulika kwamba hali halisi ya dunia haikuwa hivyo. Duniani kulikuwa kumetanda giza lililosababishwa na wanadamu. Watu hao walikuwa wamejitangazia sera zao za maisha zinazoongoza kwenye mangamizo na kifo chao wenyewe binadamu.

Binadamu walikuwa wanakandamizana, kuoneana, wanachukuana utumwa, wanatawalana ovyo, hasahasa viongozi. Hata mwandishi mmoja wa kitabu cha Daniele katika Biblia aliandika: “Wakuu wote wa dunia ni wanyama.” Aidha kulikuwa na umahuru uliokithiri ambao haukumtambua tena mwumbaji wa Nuru. Wengine walidiriki hata kujiita miungu katika nafasi zao za maisha. Mbaya zaidi watu hao walikuwa wamebobea gizani kiasi hata cha kuichukia Nuru. Kila kitu kilikuwa kinaendeshwa gizani. Anayejaribu kuwasha walau mshumaa au koroboi huyo anakuwa adui.

Basi baada ya mapitio hayo, mkutano ukabidi utoe maamuzi mazito na ya haraka. Mkutano ukawa na kazi moja tu na iliyopata kauli mbiu: AZIMIO – DUNIA. Hatimaye uamuzi uliofikiwa wa mkutano ni kuituma nafsi ya pili ya Halmashauri kuu aende duniani. Kwa bahati nzuri nafsi hiyo ikakubali kutumwa kuja missioni kwenye sayari hiyo pekee anayokaa binadamu. Ujio wa kijana huyo ulikuwa ni breaking nyuzzzz kwa wakazi wa sayari dunia hasahasa kwa wanyonge. Zilikuwa ni nyuzzz kwa sababu jambo kama hilo hawakuwahi kuliotea ndoto, kwa vile halijawahi kusikika wala kutokea popote na halitatokea tena katika historia ya binadamu eti “Mungu azaliwe”. Aidha, hakuna hata dini moja hapa duniani iliyowahi kuwa na ujasiri wa kutangaza AZIMIO kama hilo la “Mungu kuwa binadamu.”

Hiyo ndiyo kufuru na ukafiri uliobobea kudai kuwa Mungu anaweza kuzaliwa na kuwa binadamu kama binadamu wengine. Hata wayahudi wenyewe waliokuwa wamebobea katika dini walikiita kituko hicho kuwa ni Kikwazo. Kadhalika wataalamu wa filosofia waliowahi kutokea hapa duniani wanaothibitisha kabisa kwamba yuko Mungu mmoja, nao pia hawakuwa na ujasiri wa kudai kwamba Mungu anaweza kuwa binadamu, akae pamoja na binadamu na kushirikiana na binadamu. Fikra hiyo haiingii kichwani na ni kitendo cha kumdhalilisha Mungu. Kwamba haiwezekani kitu kilicho kikamilifu kabisa kama Mungu kichukue hali ya ukiumbe, kiwe na mwili ulio na mipaka na udhaifu. Wagiriki walio magwiji wa filosofia kitendo hicho walikiita ni Upuuzi.

Kwa upande wa Halmashauri Kuu, Utatu ulitegemea Nuru hiyo ingepokewa kwa kishindo hasa na watu waliobobea katika imani kwa Mungu mmoja, na wale wataalamu wa filosofia kwa vile wanaupana wa kuelewa mambo. Kumbe ikawa kinyume “Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea” (Yoh. 1:11). Mtazamo huo hasi na wa ukosoaji wa ujio wa nafsi hiyo ya pili duniani, umedumu miaka elfu mbili na unaendelea. Mbaya zaidi ikaja kugundulika kwamba AZIMIO – DUNIA likaundiwa vyama vingi vya upinzani hapa duniani. Hata hivyo, utekelezaji wa AZIMIO ulipofika, Nafsi hiyo ya pili akazaliwa kwa sababu: “macho ya chura hayawezi kumzuia ng’ombe kunywa maji.” Kuthibitisha hilo unaona hata mpangilio wa nyakati hapa duniani umepangwa kutokana na ujio wake Yeye.

Kila tunapotamka mwaka katika historia tunasema Kabla au Baada ya kuzaliwa Kristu. Swali linalowakanganya baadhi ya wakazi na wataalamu wa dunia juu ya Mungu kuwa binadamu, linapata jibu kutokana na msemo mmoja wa kilatini wa Mababa wa Kanisa unaoanisha hilo: "Quod erat permansit; quod non erat assumpsit," yaani, “Kile kilichobaki kama kilivyokuwa hata baada ya kujiunga na kile ambacho hakikuwepo.” Mungu kwa kuchukua Mwili na kuzaliwa, anabaki kuwa kama alivyokuwa kabla yake. Anabaki kuwa Mungu na sifa zake zote za kimungu: yaani anabaki kuwa Mungu mmoja, wa Milele, Mwenyezi, asiye na mwanzo wala mwisho, yupo pahala pote, habadiliki, ni mkuu daima nk. Alikuwa ni kila kitu, alijua kila kitu, aliweza kila kitu, na aliishi katika heri pamoja na Baba. Kabla hakuwa binadamu, hakuwa dhaifu, hakuwa mdhambi. Anabaki kuwa hivyo hata baada ya kuwa binadamu.

Huyo ni NURU ya kweli ikashuka duniani kulikokuwa na giza, ikabaki kuwa NURU ili ilishinde hilo giza la dunia hii. NURU hiyo haijawahi kamwe kutokea na wala haitatokea kamwe kwa sayari nyingine za ulimwenguni zilizowahi kugundulika. Kumbe daima itabaki sayari dunia kuwa makao ya NURU. Kwa hiyo kizazi cha binadamu hakitaweza tena kujidai kuwa kama Mungu kama ilivyowahi kutokea kwa baadhi ya wafalme, wakuu na watawala kujifanya miungu na kuwataka wengine wawatumikie. Hilo kamwe halitatokea tena kwa sababu tayari Mungu mwenyewe ametuondolea uvivu kwa Yeye mwenyewe kujifanya binadamu na kuwa sawa kama sisi.

Kazi kuu ya Nuru iliyofika duniani ni kupambana na giza. Huo ni mvutano na patashika ya kudumu: “Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu. Nayo nuru yang’aa gizani, wala giza halikuiweza” (Yohane 1:4-5), yaani mapambano kati ya Nuru itokayo mbinguni na giza lililoshamiri ulimwenguni linalojiona liko katika kusambaratishwa, hivi linatafuta daima jinsi ya kuizima hiyo nuru. Mwanga au nuru hiyo ni Nyota, ambaye Majusi waliongozwa nayo toka Mashariki ya mbali. Ni Nuru inayowavuruga wale ambao walikuwa wanajisikia vizuri sana kufanya shughuli zao gizani. Wale waovu, wanaopenda zaidi giza kwani nuru inawaumbua na kunawaletea maudhi.

Kuna binadamu wengine walikuwa wanajidhania kuwa wao ndiyo nuru au myanga badala ya kuutangaza na kuutolea ushuhuda NURU halisi. Tuige mfano wa Yohane Mbatizaji aliyesema kuwa yeye ni mshuhuda tu siyo nuru, bali itafika Nuru yenyewe ambaye ni Yesu wa Nazareti. Nasi tuwe mashahidi wa Nuru na siyo kujifanya Nuru. Hiyo ndiyo Christmas!

Licha ya kushuhudia Nuru, pia tuongozwe nayo, kama unavyotuhimiza utenzi wa Zakari, “Kwa njia ya rehema za Mungu wetu, ambazo kwa hizo mwangaza utokao juu umetufikia, kuwaangaza wakaao katika giza na uvuli wa mauti, na kuiongoza miguu yetu kwenye njia ya amani.” (Luka 1:78-79). Tunahitaji kuongozwa na Nuru katika giza hili la maovu, la mapambano, la kukosa amani, na la vita. Hiyo ndiyo Noeli!

Nuru hii walianza kuiona Wachungaji waliokuwa wanachunga kondoo usiku gizani. Wachungaji hao wanawawakilisha wanyonge wote, maskini wote, walio katika giza la masumbuko. Watu kama hao waongozwe na Nuru. Hiyo ndiyo Christmas!

Tusifurahie kukaa gizani, bali tufurahi kufikiwa na Nuru, kama alivyofurahi mzee Simeon pale alipomshika huyo mtoto mikononi na kusema: “Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, uliouweka tayari machoni pa watu wote. Nuru ya kuwa mwangaza wa mataifa na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.” (Luka 1:30-32). Ama kweli yatubidi tufurahi sisi tulio katika giza la mauti na la mateso ya kila aina. Lakini tumeona Nuru kama asemavyo Mateo pale Nuru hiyo ilipoanza kuhubiri: “Watu wale waliokaa katika giza wameona mwanga mkuu, nao waliokaa katika nchi na uvuli wa mauti mwanga umewazukia.” (Mt 4:15-16).

Ndugu zangu, Ulimwengu wa leo umeshehena giza la mambo mengi. Kadhalika kuna wengi wanajitokeza kujifanya Nuru kutusaidia kuchagua iwe kiuchumi, kisiasa, kidini, nk. Hadi hujui tena ipi ni nuru ya kweli. Katika safari yetu hapa bondeni kwenye machoni, sisi tuangazwe na kuongozwa na Nuru ya kweli iliyoshuka toka mbinguni. Hii ndiyo faida kubwa ya kusherekea Kristmas kwa mkristu. Yaani kule kubahatika kujua kwamba Nuru imetwaa mwili, na kukaa kwetu, na ni Nuru inayoniangaza katika njia ya ulimwengu huu uliotanda giza. Yesu ndiye ni Nuru ya ulimwengu. Ukiipokea Nuru hiyo, na kushika sera zake, hapo utakuwa umelienzi AZIMIO-DUNIA la Utatu Mtakatifu. Utakuwa umeelewa maana yake nini kusherekea Noeli. Ndipo kweli utastahili kuimba na hata kuimbiwa pamoja na Nuru: MERRY CHRISTMAS na HERI KWA NOELI.
Tumshukuru na Tumsifu Yesu Kristu. Milele Amina.
Padre Alcuin Nyirenda OSB
Sant’Anselmo-Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.