2013-12-23 08:53:42

Mahujaji 55 kutoka Tanzania wameanza hija ya kiroho Nchi Takatifu


Changamoto katika kukoleza imani tendaji: “Simameni imara katika imani” (1Kor 16:13). Hii ndiyo dira na mwaliko wa Kanisa kwa nyakati zote, na zaidi sana katika wakati wetu huu wa kihistoria ambapo kumejitokeza sana kuyumba kwa imani miongoni mwa waamini na hivi kuamsha uhitaji wa Uinjilishaji Mpya na wa kina kwa matendo.
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani lilipenda kuwashirikisha waamini tafakari ya kina kuhusu Imani ili iwaongoze wana familia ya Mungu ”katika kuishi kiaminifu imani ile tunayoishiriki pamoja, imani ambayo baada ya kuipokea tunapaswa kuilinda, kuitunza na kuikuza. Tunataka mtambue siku zote kuwa sisi, kwa wajibu tuliopewa na Kanisa, tunapaswa kufundisha, kuilinda na kuifanya imani yenu ikue, na wala “si kwamba tunatawala imani yenu; bali tu wasaidizi wa furaha yenu; maana kwa imani yenu mnasimama” (2Kor 1:24).
Ni sala yetu kuwa, katika Mwaka huu wa Imani, tutafanya bidii ya makusudi kuijua, kuiishi na kuwashirikisha wengine imani yetu, ili “sote tuufikie umoja wa imani na kumjua Mwana wa Mungu; tuwe watu waliokomaa na kuufikia utimilifu wake Kristo mwenyewe” (Efe 4:13).
Baada ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani nchini Tanzania, kundi la mahujaji 55 kutoka Tanzania limeondoka Jijini Dar es Salaam, Jumapili tarehe 22 Desemba 2013 kuelekea Nchi Takatifu na Misri, ili kukoleza imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, tayari: kuikiri, kuiadhimisha katika Liturujia na Sakramenti za Kanisa; kwa kuimwilisha katika maisha adili yanayoongozwa kimsingi na Amri za Mungu pamoja na kuimwilisha katika Sala, kielelezo cha imani tendaji!
Mahujaji kutoka Tanzania wanatembelea maeneo ya historia ya ukombozi kadiri ya Maandiko Matakatifu: Wanatembelea eneo alilozaliwa Yesu; mahali alipoteswa, akafa na kufufuka. Kipindi hiki kuanzia tarehe 23 Desemba hadi tarehe 31 Desemba 2013, utakuwa ni muda wa sala na tafakari ya Neno la Mungu. Kundi la mahujaji kutoka Tanzania linaongozwa na Padre Desiderius Rugemalira, Paroko wa Parokia ya Kilimahewa, Jimbo kuu la Dar es Salaam. Linawajumuisha Mapadre 5, Watawa 7 na wengine wote waliobaki ni Waamini walei kutoka Majimbo mbali mbali ya Kanisa Katoliki nchini Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.