2013-12-21 07:44:13

Wanafunzi zingatieni maadili na utu wema!


Mafanikio makubwa yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino cha Tanzania, SAUT ni mchango wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika maboresho ya sekta ya elimu. RealAudioMP3

Lengo ni kuwajengea wahitimu fursa za kuweza kupata ajira sanjari na kupambana na changamoto zinazojitokeza katika maisha. SAUT inapania kuwaandaa waatalam wenye maadili, utu wema, ari na moyo wa kujituma ili kushiriki katika mchakato wa ujenzi wa Jiji la Mungu.

Ni changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Askofu Evaristi Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya, Tanzania, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo Kikuu cha SAUT, Tawi la Mbeya wakati wa Ibada ya Misa Takatifu kama sehemu ya ufunguzi rasmi wa Mwaka wa Masomo 2013-2014. Zaidi ya wanafunzi 350 wamejiunga na SAUT, Tawi la Mbeya kwa kozi mbali mbali zinazotolewa Chuoni hapo.

Askofu Chengula imeitaka Jamii kuendeleza maadili na utu wema kwa kuwaonesha wanafunzi hao ukarimu pamoja na kuwajengea mazingira mazuri yatakayowasaidia kujikita zaidi katika masomo, daima wakijiandaa kwa maisha bora kwa siku za usoni. Amewataka wanafunzi kusimama kidete kulinda na kudumisha Injili ya Uhai dhidi ya utamaduni wa kifo unaokumbatia sera za utoaji mimba, hali inayowatendea sana kwa kuwaacha katika utupu na majonzi na madonda ya muda mrefu.

Wakati huo huo, Professa Romwald Haule amewataka wanafunzi kujifunza kwa bidii, juhudi na maarifa, huku wakionesha moyo wa unyenyekevu, kwani elimu wanayoipata wakati wakiwa chuoni ni tone tu la maarifa yanayoweza kupatikana duniani.








All the contents on this site are copyrighted ©.