2013-12-21 09:40:27

Ujumbe wa Noeli kwa Mwaka 2013 kutoka kwa Patriak Fouad Twal wa Yerusalemu


Katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka 2013, Kanisa linapenda kuonesha mshikamano wa dhati na wananchi wa Syria wanaoendelea kuteseka kutokana na vita na kwamba, kuna maelfu ya watu yamelazimika kuyakimbia makazi yao kutokana kuhofia kuhusu usalama wa mali na maisha yao! Hili ni kundi ambalo linalazimika kuishi kama wakimbizi katika nchi jirani ziliko kwenye Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Kanisa kwa upande wake, litaendelea kuombea amani, upendo na mshikamano wa dhati kati ya watu sanjari na kutoa msaada wa hali na mali kwa waathirika wa vita na kinzani za kijamii, kisiasa na kidini huko Masharki ya Kati.

Katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, Kanisa limeendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekumene, jambo ambalo linaendelea kuzaa matunda ya ushirikiano yanayoonekana kati ya waamini wa dini na madhehebu mbali mbali ya Kikristo.

Waamini wanaoishi huko Mashariki ya Kati, wana matumaini makubwa ya kukutana na kuonana na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kichungaji katika Nchi Takatifu. Hii itakuwa ni fursa nyingine ya kuweza kuwaimarisha ndugu zake katika imani, mapendo na matumaini, licha ya magumu wanayokabiliana nayo katika hija ya maisha na utume wao kama Wakristo huko Nchi Takatifu. Wapalestina na Waisraeli wana haki ya kuishi katika Nchi Takatifu.

Huu ni ujumbe wa Patriaki Fouad Twal wa Yerusalemu katika maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli kwa Mwaka 2013. Ni ujumbe unaotoa kwa muhtasari matukio makubwa yaliyojiri katika Kipindi cha Mwaka 2013 unaoyoyoma kwa kasi! Maadhimisho na kufunga Mwaka wa Imani; mateso na mahangaiko ya wananchi wa Syria, Iraq, Libya na Misri bila kusahau mgogoro wa siku nyingi kati ya Israeli na Palestina na umuhimu wa kutafuta amani ya kudumu huko Mashariki ya Kati kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watu wake.

Patriaki Fouad Twal anawaalika wanasiasa kuonesha utashi wa kisiasa, ili kuweza kutafuta suluhu ya kudumu kwa kusitisha vita ambayo imeendelea kusababisha madhara makubwa kwa maisha na mali ya watu; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu, kinyume kabisa na mwelekeo wa sasa unaokumbatia utamaduni wa kifo na madhulumu!

Patriaki Twal anasema, kwa mara ya kwanza Kanisa Katoliki na Kanisa la Kiorthodox waliweza kuadhimisha Pasaka siku moja, hapo tarehe 5 Mei 2013, hii ni hatua kubwa katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene miongoni mwa Makanisa katika masuala ya imani, ili hatimaye, kufikia umoja kamili kadiri ya mapenzi ya Kristo kwa Kanisa lake.

Patriaki Twal analaani vitendo vyote vinavyosababishwa na waamini wenye misimamo mikali ya kidini inayoendelea kuongezeka siku hadi siku kutokana na chuki za kidini, jambo ambalo halipendezi kwani linatishia uhuru wa kuabudu ambao ni sehemu ya haki msingi za binadamu. Kanisa katika Nchi Takatifu, litaendelea kuwekeza katika sekta ya elimu na kuboresha makazi ya Familia za Kikristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.