Pendekezeni majina ya watu watakaoshiriki katika Bunge maalum la Katiba
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete ameyaalika na kuyakaribisha
makundi mbali mbali katika jamii kupendekeza majina ya watu ambao Rais atayafikiria
katika uteuzi wa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba. Rais Kikwete ametoa mwaliko huo
kulingana na mamlaka anayopewa katika Kifungu cha 22(1) (c) cha Sheria ya Mabadiliko
ya Katiba (Sura ya 83) na aliutangaza rasmi mwaliko huo katika Gazeti la Serikali
Na. 443 la Ijumaa iliyopita, Desemba 13, 2013.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa
Dar es Salaam Ijumaa, Desemba 20, 2013 na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue,
mwaliko huo ambao pia utatangazwa katika magazeti ya kawaida, makundi yaliyokaribishwa
kutoa mapendekezo yametakiwa kuwasilisha kwa Rais orodha ya watu wasiopungua wanne
na wasiozidi tisa kwa kila kundi.
Makundi hayo ambayo yametajwa katika Sheria
ya Mabadiliko ya Katiba ni Taasisi zisizokuwa za Kiserikali, Taasisi za kidini, Vyama
vyote vya siasa vyenye usajili wa kudumu, Taasisi za elimu ya juu, Makundi ya watu
wenye ulemavu, Vyama vya wafanyakazi, Vyama vinavyowakilisha wafugaji, Vyama vinavyowakilisha
wavuvi, Vyama vya wakulima na Makundi mengine yenye malengo yanayofanana.
Taarifa
ya Balozi Sefue inasema kuwa katika kuwasilisha mapendekezo ya majina yao, makundi
yaliyoalikwa yanalazimika kuonyesha umri, jinsia, uzoefu, sifa na sehemu ya makazi
ya mtu anayependekezwa ikiwa ni pamoja na kuzingatia usawa wa kijinsia. Katika mwaliko
wake, Rais Kikwete ameelekeza kuwa orodha ya majina ya wanaopendekezwa, iwasilishwe
kwa maandishi ama kwa kupelekwa na mtu kwa mkono ama kwa kutumia huduma ya Posta.