2013-12-21 11:53:08

Mtikisiko wa kisiasa nchini Tanzania!


Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania amebariki maamuzi ya wabunge na kutengua nyadhifa za mawaziri wanne wa Baraza la Mawaziri kufuatia kashfa ya Operesheni Tokomeza Majangili na Operesheni Kimbunga. Hii ni mara ya tatu kwa Baraza la Mawaziri la Rais Jakaya Kikwete kujiuzulu kufuatia kashfa mbalimbali katika kipindi cha mwaka 2008 – 2013.

Uamuzi wa kujiuzulu kwa mawaziri hao ulitangazwa jana Bungeni na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, baada ya aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, kusimama bungeni na kutangaza mwenyewe kujiuzulu na kufuatiliwa na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. David Mathayo, ambaye pamoja na kutakiwa na wabunge ajiuzulu, aligoma kutangaza uamuzi huo.

Rais Kikwete alitoa uamuzi huo akiwa nchini Marekani kwa matibabu baada ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kumpelekea maoni yaliyotolewa na wabunge.
Waliowajibishwa ni Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. Mathayo David, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki , Waziri wa Mambo ya Ndani Dk. Emmanuel Nchimbi na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha.

Hata hivyo, Dk. Nchimbi na Waziri wa Ulinzi, Nahodha, hawakuwepo ukumbini , wakati uamuzi huo ukitolewa. Hatua ya Rais ilitangazwa Ijumaa saa 2:30 usiku bungeni na Waziri Mkuu Pinda , aliyekuwa anatoa msimamo wa serikali kuhusiana na hoja hiyo ya kuwawajibisha kutokana na uovu uliofanywa na watekelezaji wa operesheni hiyo uliosababisha mauaji ya watu 19.

Waziri Mkuu ambaye naye alitakiwa na wabunge kujiuzulu hakuwa tayari kujizungumzia wala kujibu hoja zilizomtuhumu. Alisisitiza kuwa operesheni hiyo imesimamiwa na wizara tatu za Maliasili na Utalii, Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Mambo ya Ndani hivyo awali alizungumza na mawaziri wote wanne na kukubalina kuwa katika mazingira hayo na kauli za wabunge walizoshauri wachukulie kwa msingi kuwa ni busara wakubali ushauri wa Bunge wakukubali kuwajibika.

“Waheshimiwa wote wanne wamekubali kujiuzulu na kilichofanya walikubali kufanya hivyo ni kwamba vyombo vilivyohusika viko chini ya usimamizi wao.”

DK. MATHAYO
Akizungumzia Dk. Mathayo alisema kwa maana ya operesheni tokomeza ni vigumu kusema kuwa alihusika moja kwa moja kwani hakuwa na vyombo vilivyosimamia operesheni hiyo na kwamba hakuhusika na vitendo vilivyojitokeza . Lakini kwa msingi huo alitakiwa kujiuzulu kwa kuwa anasimamia Wizara ya Mifugo na ambayo inaweza kuchukuliwa kuwa alishindwa kusimamia mifugo ambayo imeingia kwenye hifadhi. “Nilimueleza kuhusu Mathayo kuwa anaweza asihusike moja kwa moja na operesheni tokomeza lakini pengine aangaliwe kama yeye ni msimamizi wa mifugo. Hii inaweza kuchukuliwa kuwa ndiyo maana ameshindwa kusimamia mifugo inayoingia kwenye hifadhi za taifa”. Alichosema hapana ni kwamba hakuna haja ya kugombana kwenye jambo hilo ambalo ni kubwa hivyo si vibaya na yeye akaliona kwa mtizamo huo na kujiuzulu kama wengine.

TUME

Akizungumzia kuhusu kuundwa kwa tume aliongea na Rais na hilo ameliunga mkono na kushauri tume iundwe na matokeo yake yapatikane kwa muda mfupi ili watendaji wote waliohusika bila kujali ni wa ngazi gani au taasisi gani wachukuliwe hatua za kisheria na kinidhamu.

RIPOTI

Akiizungumzia matukio yaliyoibuliwa na kamati hiyo ya unyanyasaji, udhalilishaji na mauaji ya watu na mifugo haukubaliki na serikali itachukua hatua. Na kusisitiza kuwa kikwazo kikubwa ni namna operesheni iliyotekelezwa na kusimamiwa. Aliwataka mawaziri hao waone kuwa ni sehemu ya jukumu lao na anakubaliana na wabunge wanaotaka mawaziri wabebe lawama kwa hiari yao wenyewe.
Nimejaribu kutizama maelezo yaliyotolewa taarifa hizo zinahitaji kuthibitishwa zaidi. Ushauri wa Mwanasheria umezingatia zitakuwepo hatua za kiutawala na za kisheria.

Kuna uvunjifu mkubwa wa sheria na kunahitajika tume ya kimahakama kuwachunguza ili wahusika washughulikiwe, naamini muda mfupi kadri ya mwezi mmoja tupate taarifa ya uchunguzi na hatua kwa kila mmoja zichukuliwe.
Hata hivyo alisisitiza umuhimu wa kutunza mali asili hasa wanyama pori akieleza kuwa sensa inaonyesha kuwa katika hifadhi ya Selous kulikuwa na 55,000 lakini sawa wamebakia tembo 13,000.


WAZIRI KAGASHEKI AIBUKA SHUJAA
Akitoa maelezo ya kujiuzulu bungeni Balozi Kagasheki alisema “mimi ni mtu mzima nimesikia hisia na sauti za wabunge na mimi nasema .. Mheshimwa Rais Dk. Jakaya Kikwete, aliponiteua ilikuwa ni katika furaha yake naamini kabisa aliniamini kuwa ningeweza kufanya kazi kama alivyotegemea” “Lakini kutokana na operesheni hii kuna mabaya yametokea naamini uchunguzi utafanyika kuwafahamu waliohusika….niombe tu nimeseme kuwa mimi mwenyewe nimewasikia kwa kauli yangu natamka wazi kuwa ni nia yangu kushuka ngazi hii ya uwaziri, ninajiuzulu.”

Alisema na kushangiliwa na Bunge na kuahidi kuwa atachukua hatua ya kuzitaarifu mamlaka zilizompa jukumu hilo.

Mathayo ‘ninaonewa’Alilalamika kuwa anahukumiwa kuwa mtuhumiwa bila kuhojiwa. Alisema ripoti nzima haikutaja kuwa amehusika na operesheni tokomeza na kuongeza kuwa hakuitwa kuhojiwa na kamati na kwamba hajawahi kuona mahakama inayomhukumu mshitakiwa bila kumhoji. Alisisitiza kuwa ameonewa na Mungu mwenyewe atawashughulikia hao wanaotaka ang’oke na kwamba alikuwa anasali zaburi ya 72.

Aliiponda ripoti hiyo ya kamati kwa kutoa taarifa za uongo kuwa Tanzania ni nchi ya pili kwa mifugo lakini haina sera na mipango ya muda mrefu ya kuendeleza mifugo. Alisema sera ipo na ilipitishwa na Bunge mwaka 2006 na pia kuna mipango ya muda mrefu na mfupi ya kuendeleza mifugo. “Kwangu haingii akilini mimi kuambiwa sina sera sina mipango , alisema na kujitetea kuwa matatizo ya sekta ya mifugo ni ya kitaasisi”.








All the contents on this site are copyrighted ©.