2013-12-21 12:13:42

AMECEA yasikitishwa na kuzuka kwa vita ya wenyewe kwa wenyewe nchini Sudan ya Kusini


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na kati, AMECEA limepokea kwa masikitiko makubwa machafuko ya kisiasa na kijamii yanayoendelea nchini Sudan ya Kusini na hivyo kusababisha maafa makubwa kwa watu. Ni matumaini ya AMECEA kwamba, hali hii itaweza kupatiwa ufumbuzi wa haraka, ili haki, amani, upendo na mshikamano viendelee kutawala miongoni mwa wananchi wa Sudan ya Kusini.

Inasikitisha kuona kwamba, baada ya vita ya wenyewe kwa wenyewe kutawala nchini Sudan kwa miaka arobaini na hatimaye, kura ya maoni ikapigwa na Sudan ya Kusini ikapewa uhuru kamili wa kujiamlia mambo yake, imerudi tena katika vita ya wenyewe kwa wenyewe! Mwaka mmoja wa uhuru wa Sudan ya Kusini, unapaswa kuwa ni kipindi cha kujijenga na kujiimarisha katika mapambano dhidi ya ujinga, maradhi na kuweka mikakati ya maendeleo endelevu kwa ajili ya ustawi wa wananchi wa Sudan ya Kusini na wala si kujikita katika vita!

Ni maneno ya Askofu mkuu Tarcisius Zizaye, Rais wa AMECEA wakati huu Jumuiya ya Kimataifa inapoyaelekeza macho yake Kusini mwa Sudan. AMECEA inaendelea kutolea sala zake, ili amani na upatanisho viweze kupatikana tena Sudan ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.