Mshikamano kwa njia ya sala kama sehemu ya Maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi maalum
ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, 2014
Baba Mtakatifu Francisko ameandika sala maalum kwa ajili ya Familia, kama sehemu ya
Maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayoadhimishwa
Mwezi Oktoba 2014. Sala hii itatolewa rasmi na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa
Sala ya Malaika wa Bwana, hapo tarehe 29 Desemba 2013 wakati wa Maadhimisho ya Siku
kuu ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu.
Baba Mtakatifu Francisko
katika tukio hili anatarajiwa kuungana na waamini watakaokuwa wanasali kwa ajili ya
kuombea Familia mjini Nazareth na Loreto. Askofu mkuu Lorenzo Baldisseri, Katibu mkuu
wa Sinodi za Maaskofu ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Kupashwa
habari za kuzaliwa kwa Bwana mjini Nazareth na Askofu mkuu Giovanni Tonucci, ataadhimisha
Ibada ya Misa Takatifu kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Loreto.
Zote hizi
ni jitihada za mchakato wa maandalizi kwa ajili ya Maadhimisho ya Sinodi maalum ya
Maaskofu kwa ajili ya Familia itakaoadhimishwa kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba
2014, kwa kuongozwa na kauli mbiu " Changamoto za kichungaji katika familia mintarafu
Uinjilishaji".
Kwa lengo hili hili, Askofu mkuu Vincenzo Paglia, Rais wa Baraza
la Kipapa kwa ajili ya Familia, hapo tarehe 22 Desemba 2013 anatarajiwa kuadhimisha
Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Familia Takatifu, Jimbo kuu la Barcelona.